May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Mkuu awapa somo Mawaziri,Manaibu Mawaziri

Na Joyce Kasiki,Timesmajira.online,Dodoma

WAZIRI MKuu wa Jamhuri yaMuungano wa Tanzania Kassim Majaliwa amewataka Mawaziri na Manaibu Mawaziri kutunza siri za Serikali hasa katika kipindi hiki cha utandawazi huku akiwataka kuacha matumizi ya wasaidizi binafsi wanaowatumia kuwafanyia kazi katika ofisi za Umma.

Akifungua mafunzo ya siku kwa viongozi hao yaliyoandaliwa na Taasisi ya Uongozi na kufanyika  jijini hapa,Majaliwa amesema,katika kipindi hiki kumekuwa na uvujaji wa siri za Serikali katika mitandao ya kijamii jambo amesema siyo sahihi kwa Taifa.

“Utunzaji wa siri za Serikali ni muhimu kwenu hasa kipindi hiki cha utandawazi,tumetumeshuhudia barua za siri za Serikali zikisambaa katika mitandao ya kijamii,naomba hili mkalisimamie hatupendi kuona likiendelea.”amesema Majaliwa

Amesema,matumizi ya walinzi na wanahabari binafsi katika ofisi za umma kunasababisha kuvuja kwa siri za Serikali huku akisema upo utaratibu wa kufuata iwapo itabainika m,nahitaji kupatiwa wasaidizi hao huku akiwataka kuzingatia utaratibu huo na siyo vinginevyo.

Vile vile amewataka kuwa na lugha zenye staha,kusimamamia suala la Utawala bora kwa kukemea vitendo vya rushwa ,ubadhirifu wa mali na fedha za umma.

“Pia mnapaswa kuunga mkono matamko ya viongozi wakuu ambao ni Rais,Makamu wa Rais na Waziri Mkuu ,sikiliza kwa makini kama kuna jambo la wewe kulifanyia kazi ulichukue na kuanza utekelezaji wake,usisubiri uandikiwe barua ya kutekeleza jambo fulani,hatuwezi kuandika barua kwa kila mtu.”amesema Majaliwa na kuongeza kuwa

“Iwe ni kampeni mbalimbali au tamko lolote linalotolewa ,lazima mliunge mkono ,kwa mfano tutakumbuka hivi karibuni Rais Samia Suluhu Hassan alizindua kampeni ya mapambano dhidi ya UVIKO 19 ,pia alifanya uzinduzi wa Sensa ya Watu na Makazi inayotarajia kufanyika mwakani ,yote haya lazima tuyaunge mkono kwa kuyazungumza kwa wananchi ili kuhamasisha wananchi kushiriki kikamilifu.”

Kwa upande wake Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma Mohamed Mchengerwa ametumia nafasi hiyo kuziagiza Wizara,Idara na Taasisi zote za Serikali kuhakikisha zinatenga bajeti kwa ajili ya kuwapeleka watumishi kushiriki katika mafunzo yanayotolewa na Taasisi ya Uongozi Nchini ambayo yana lengo jema la kujenga uwezo wa watumishi hasa viongozi ili kuboresha utendaji wao.

Awali Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi Kadari Singo amesema lengo la mafunzo kwa viongozi hao ni kuongeza uelewa wao ili kuboresha utendaji wao.

Aidha amesema katika miaka michache iliyopita tayari wametoa mafunzo hayo kwa viongozi mbalimbali wapatao 8,000.