April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Dkt. Gwajima: Sensa 2022 tusiwaache wazee wetu

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima, ameitaka jamii kulikumbuka kundi la Wazee wakati wa Sensa ya Watu na Makaazi itakayofanyika Agosti 23, 2022 ili nao waweze kuingizwa kwenye mipango ya taifa.

Dkt. Dorothy Gwajima ametoa kauli hiyo leo Juni, 10, 2022, jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa Habari kuelekea Siku ya kupinga ukatili kwa Wazee Duniani itakayo adhimishwa Juni 15, 2022.

Dkt. Gwajima ameongeza kuwa Nikupitia takwimu za Sensa pekee ndio zitaweza kusaidia kupanga mipango mizuri ya nchi, hivyo tunapokwenda kuadhimisha siku hii iliyobebwa na na kaulimbiu “Tuhakikishe wazee wanalindwa, wanasikilizwa na kuheshimiwa, tusikose kuhesabiwa kwenye Sensa ya Watu na Makazi.

“Ni imani yangu kila mmoja kwa nafasi yake atakuwa msatari wa mbele kuhimiza zoezi la sensa ka makundi yote likiwepo kundi hili la wazee” alisema Dkt. Gwajima

Dkt. Gwajima alisema lengo la maadhimisho hayo ni kuelimisha jamii kuhusu kupinga ukatili wa aina zote dhidi ya Wazee ambao ni ukatili wa kimwili, kihisia na kiuchum sambamba na kuelimisha jamii juu ya changamoto mbalimbali zinazowakabili Wazee zinazotokana na mila na desturi potofu, fursa walizonazo na masuala ya uzee na kuzeeka.

“ Kwa mijibu wa jeshi la Polisi katika kipindi cha Januari hadi Desemba, 2020 kulikuwa na matukio 54 ya kuuawa kwa wazee nchini, lakini katika kipindi cha Januari hadi Desemba, 2021 hapakuwepo na tukio lolote la kuuawa kwa wazee nchini Aidha, kwa kipindi cha Januari hadi Juni, 2022 kumetokea matukio kwenye Mkoa wa Singida, Wilaya ya Iramba la mauaji ya wazee watatu (3) wanawake kwa kuhusishwa na imani za kishirikina, hii haikubaliki, alisisitiza Dkt. Gwajima.

Dkt. Gwajima amefafanua kuwa katika kukabilina na changamoto hiyo Serikali imeunda mabaraza ya wazee kuanzia ngazi ya kijiji hadi Taifa ambapo yako takribani 20,749, mabaraza hayo kwa kushirikiana na wadau ili yatumike kutoa elimu kuhusu ukatili dhidi ya wazee.

Katika hatua nyingine Waziri Dkt. Gwajima, ameitaka jamii, kuendelea kujiunga kwenye kampeni ya SHUJAA WA MAENDELEO NA USTAWI WA JAMII (SMAUJATA) kupitia kiungio cha https://forms.gle/DtGthrUTLhXJp2cUA pia kwenye mtandao wa kijamii wa Telegram kwa link; https://t.me/+IFypK6_FB-k30TIk. Kwa upande wa Instagram ni @smaujata.tz.

Tarehe 15 Juni ya kila mwaka Dunia inaadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupinga Ukatili dhidi ya Wazee. Siku hii huadhimishwa kufuatia Azimio la Umoja wa Mataifa Na. 66/127 la Desemba 2011 lililotokana na maombi ya Shirika la Mtandao wa Kimataifa wa Kuzuia Ukatili dhidi ya Wazee.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima, akizungumza na waandishi wa Habari jijini Dar Es Salaam, kuelekea Siku ya kupinga ukatili kwa wazee Duniani inayofanyika Juni 15, kila mwaka.
Baadhi ya Waandshi wa Habari, wakiwa kazini kufuatilia taarifa kwa Umma kutoka kwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima, kuelekea Siku ya kupinga ukatili kwa Wazee inayofanyika Juni 15, kila mwaka.
(Picha zote na kitengo cha Mawasiliano Serikalini WMJJWM)