March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Simbachawene:Jumla ya Tani 1.13 za heroin zilikamatwa nchini 2021

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

WAZIRI wa nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu(Sera,Bunge na uratibu) George Simbachawene amesema kuwa kwa mara ya kwanza mwaka 2020  katika historia ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini shehena kubwa ya jumla ya kilo 430.77 za dawa za kulevya aina ya methamphetamine inayotengenezwa na kemikali bashirifu ilikamatwa ikihusisha watuhumiwa tisa raia wa Iran wote wakiwa wanaume.

Simbachawene amesema hayo jijini hapa leo Bungeni wakati akizungumza na Waandishi wa habari kuhusu kuwasilishwa Bungeni kwa taarifa ya hali ya dawa za kulevya kwa mwaka 2022 lengo likiwa ni kuwafahamisha wananchi hali halisi ya tatizo hilo pamoja na changamoto zilizopo katika kukabiliana nalo.

Amesema licha ya juhudi zilizopo katika kukabiliana na dawa za kulevya,bangi na mirungi zimeendelea kuwa tatizo ambapo mwaka 2021 jumla ya tani 22.74 za bangi zilikamatwa ikiwa ni ongezeko la asilimia 72 ya kiasi kilicholamatwa mwaka 2020.

Huku kwa upande wa mirungi iliyokamatwa katika kipindi hicho ilifikia tani 10.93 zikihusisha watuhumiwa 1395 na kuelezwa kuwa dawa za kulevya zinazozalishwa viwandani mwaka 2021 jumla ya tani 1.13 za heroin zilikamatwa.

“Hiki ni kiasi kikubwa sana kuwahi kukamatwa kwa mwaka mmoja katika historian ya nchi yetu,kiasi hiki ni mara tatu ya kiasi kilicholamatwa mwaka 2020 na katika kipindi hicho kiasi cha gramu 811.30 za cocaine zilikamatwa,

“Katika kukabiliana na hilo Serikali inaendelea kufuatilia mwenendo wa uingizwaji na matumizi ya methamphetamine pamoja na kemikali bashirifu ambazo hutumika kutengeneza dawa hizo,”amesema

Amesema pamoja na juhudi nyingi za udhibiti wa dawa za kulevya,hadi kufikia mwezi desemba 2021 waraibu wa dawa mbalimbali za kulevya pamoja na vilevi vingine wapatao 905,902 walijitokeza kupata tiba katika hospitali za Wilaya na mikoa nchini.

Hata hivyo amesema Serikali imeendelea kupanua wigo wa matibabu kwa waraibu wa dawa za kulevya ambapo hadi kufikia mwezi desemba 2021 huduma za tiba ya uraibu zilikuwa zikipatokana katika vituo 15 vya kutolea tiba kwa waraibu wa heroini ambapo vituo hivyo kwa pamoja vilisajiri waraibu 11,650.

“Vituo hivi vinapatikana Katika mikoa ya Dar Es Salaam,Pwani,Tanga,Mbeya,Songwe , Dodoma,Mwanza na Arusha,vilevile Serikali itaendelea kufanya usimamizi Katika nyumba 44 za upataji nafuu nchini ambapo nyumba hizi huanzishwa na kuendeshwa na asasi za kiraia na Serikali kwa kupitia mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya imetengeneza mwongozo wa uanzishaji na uendeshaji nyumba hizo,”amesema

Kwa upande wake Kamishna jenerali wa mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya nchini Gerald Kusaya amesema pamoja na kuhamasisha jamii kukabiliana na tatizo hilo akiwataka wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali kwa kuwabaini wanaouza au kusambaza dawa za kulevya kwa namna yoyote.

Amesema,mapambano dhidi ya dawa za kulevya bado yanahitaji sheria madhubuti ili iweze kutoa matokeo bora
Kwa kuwabana na kuwawajibisha wale wote wanaojihusisha na biashara hiyo  haramu .

“Kwa kuhakikisha hilo linafanikiwa sheria imekuwa ikiboreshwa mara kwa mara ili kudhibiti kikamilifu tatizo la dawa za kulevya na kuifanyia marekebisho kila inapohitajika,”alisisitiza Kusaya