May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wazazi watakiwa kupeleka watoto nje ya nchi

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Wazazi wametakiwa kuhakikisha wanawapeleka watoto wao kushiriki katika safari za nchi za nje ili waweze kupanua mawazo, kujifunza zaidi na kuwa na mchango kwa Taifa na wao wenyewe.

Hayo ameyasema
Mkuu wa shule ya Dar es Salaam independent School, Catherine Shindika wakati akizingumza na waandishi wa Habari juzi jijiji Dar es Salaam akiwasafirisha wanafunzi wa shule hiyo kwenda katika nchi ya ufaransa na Spein ikiwa ni safari ya 15 tangu kuanza kwa safari hizo ambapo watakaa kwa wiki 2 lengo ikiwa ni kujifunza na kuwapanua kimawazo.

Shindika amesema safari hizo huandaliwa Kila mwaka na wanazitoa kuanzia Darasa la 6 mpaka form 6 ambazo mzazi huzilipia, kwani wanaamini kwamba mtoto akipewa nafasi ya kujifunza atagundua vitu ambavyo hata mwalimu havijui.

“Kawaida hizi safari tunaziadaa Kila mwaka na hii ni safari yetu ya 15 kwenda nchi za nje ili kuwapa watoto mwanga na mwangaza kwasababu pia mtaala wetu unahitaji watoto wapanuliwe mawazo na siyo washindiliwe”

“Tunapoandaa safari kama hizi tunawapa nafasi ili waweze kuona na kujifunza zaidi huko wanakokwenda katika nchi za wenzetu ili watakaporudi nao wawe na mchango kwa Taifa na wao wenyewe” Amesema Shindika

Aidha Shindika amesema walipoanza safari hizo walikua wakienda nchi ya ufaransa pekee kwasababu ndiyo lugha ya Kimataifa wanayoifundisha shuleni hapo lakini kwa sasa wamepanua safari hizo na kwenda nchi nyingine ikiwemo Ujerumani, uswis na Italy.

“Nchi tunazowapeleka ni Shenghen na safari hii tunaenda nchi ya uhispania spein na ufaransa, na tulipoanza tulikuwa tunaenda ufaransa pekee kwasababu ndiyo lugha ya Kimataifa tunayoifundisha pale shuleni, Wanafunzi wanaenda kupanua mawazo, kuona mandhari ya nchi hizo lakini pia lugha.

Mkuu huyo wa shule amesema safari hizo zilisimama kwa muda kutokana na janga la COVID-19 ambapo kwa sasa wameanza tena ambapo wazazi wamejitokeza kwa wingi kuleta watoto wao kushiriki safari hii.

“Tumeshazialika shule nyingine zimekwenda na sisi hivyo tunaomba hizi nafasi ziwepo na shule nyingine pia na wazazi wengine pia waone kuna haja ya kuwapeleka watoto wao”

Akizungumza mafanikio na matokeo ya safari hizo, Mkuu huyo wa shule amesema kupitia safari hizo watoto wengi wameweza kusoma nje na kupata scholarship kubwa kwasababu tayari wameshapata mwanga na wakafanya bidii na hata sasa wanakazi nzuri ndani na nje ya nchi.

Naye mwanafunzi wa kidato Cha 5 shule ya DIS, Harimat Kitendo amesema ameshiriki katika safari hiyo ili akapanue mawazo, kubadilisha mazingira na kuweza kujiongezea ujuzi.

“Mimi nataka kuwa Rubani hivyo nikifika nje ya nchi nitatafuta shule nzuri na kusoma huko Kisha kuja kuisaidia Tanzania kuijenga ndege nyingine au kusafirisha watu nchi za nje”

Allen Jacob, Mwanafunzi wa kidato Cha 3 shule ya DIS amesema Moja ya faida ya kusafiri nchi za nje ni kubadilisha mazingira na kuyajua yalivyo lakini pia kujuana na wanafunzi wengine vizuri na kujenga uhusiano.

“Ninasafiri kwasababu nimeona pale ntakapomaliza chuo ninaweza nikawa na ushawishi wa kwenda nchi nje nikajua kabisa ni mazingira gani ninaweza nikakutana nayo na nikayamudu”