September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watumishi hospitali ya Rufaa kanda ya Mbeya wafundwa juu ya mfumo wa usimamizi

Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya

WATENDAJI kutoka Idara mbalimbali za Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (MZRH) wamepatiwa mafunzo ya Mfumo wa Usimamizi wa Mali za Serikali (Government Assets Management Information System (GAMIS) ili kuwawezesha kuingiza na kuhuisha taarifa za mali za taasisi kwenye mfumo kwa wakati.

Mafunzo hayo yametolewa Julai 11,2024 na wakufunzi kutoka Wizara ya Fedha Said Mtatura na Simon Njoka mbaye pia ni msimamizi wa mali za Serikali Mkoa wa Mbeya na Songwe na kueleza kuwa mafunzo hayo ni wezeshi kwa maofisa usimamizi wa mali za Serikali hususani ambao ni wapya kwa lengo la kuwajengea uwezo kwenye matumizi ya moduli zilizopo kwenye mfumo wa GAMIS.

Mkurugenzi wa Utawala na Huduma shirikishi hospitali ya Rufaa kanda ya Mbeya,Myriam Msalale amesema kuwa mafunzo hayo ya siku 4 kwa watumishi wa hospitali hiyo yatakuwa nyezo muhimu katika kuwajengea uwezo zaidi.

Msalale amewapongeza watumishi walioshiri katika Mafunzo hayo na kutaka kuwa walimu kwa wengine kwenye programu ya GAMIS kwa matokeo ya usalama, faida na matumizi ya hospitali.

“Tumeaona faida nyingi katika mafunzo haya, matumizi sahihi ya mfumo wa GAMIS hususani moduli mama ya usajili wa mali na moduli nyingine zilizopo katika mfumo huo yanatuwezesha kutambua kiasi, idadi, hali na mali zilizopo na kuziwezesha taasisi kufunga hesabu za fedha kwa kutumia taarifa zilizopo katika mfumo wa GAMIS kama ilivyoelekezwa kupitia waraka wa Hazina Na. 2 wa mwaka 2021/2022,” amesema.

Katika jitihada za kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na kuendana na uchumi wa kidigitali, Serikali iliamua kuanzisha mfumo wa kielektroniki wa usimamizi wa mali za Serikali (GAMIS) kwa lengo la kuimarisha mfumo wa usimamizi wa mali za umma pamoja na kuondoa changamoto zilizopo.