March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watu 3,000 kushiriki Wiki ya AZAKI

Na Zena Mohamed, Timesmajira Online, Dodoma

ZAIDI ya watu 3,000 wanatarajiwa kushiriki katika Wiki ya Asasi za Kiraia (AZAKI) ambapo Asasi za kiraia 1500 zinatarajia kukutana katika wiki hiyo inayotarajiwa kuanza kufanyika oktoba 23 hadi 29 mwaka huu katika uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.

Akizungumza kwa niaba ya kamati ya maandalizi jijini hapa leo,Mwenyekiti wa kamati hiyo,Mkurugenzi Mtendaji wa Asasi ya Hakirasilimali, Racheal Chaganja amesema lengo la wiki hiyo ni kuendelea kuimarisha na kujenga mahusiano mazuri baina ya serikali,watu binafsi pamoja na Asasi za kiraia katika ujenzi wa Taifa.

Ameeleza kuwa, katika wiki hiyo kutakuwepo na mijadala na midahalo mbalimbali pamoja na maonesho ya kazi zinazofanywa na Asasi za Kiraia kama msaada wa masuala ya kisheria.

“Kwa mwaka huu wiki ya AZAKI imejipanga vyema na kwa nguvu kubwa Kwani kwa mwaka Jana hapakuwepo na maonesho kutokana na kuwepo kwa ugonjwa wa Corona jambo ambalo lilipelekea Katika kipindi hicho kujipanga vyema kwa mwaka huu,”amesema.

Ameeleza zaidi kuwa, katika wiki hiyo ya Azaki kutatanguliwa na maonesho kwa siku mbili katika viwanja vya Jamhuri ambapo yatatoa fursa kwa washirika wote kuonesha bidhaa zao zinazotokana na mashiriki yao ambapo wananchi watafika kuona bidhaa hizo na baada ya hapo siku zinazofuata ni kwa ajili ya midahalo.

“Kwa niaba ya kamati nipende kuwakaribisha Watanzania wote kwenye wiki ya AZAKI itakayo fanyika kuanzia tarehe 23 mpaka tarehe 29 mwezi Oktoba mwaka huu tumejipanga vyema kuhakikisha maonyesho hayo yanafana watu wote watapata fursa mbalimbali ya kujifunza Mambo mengi na kupata msaada wa kisheria,”amesema.

Pia amesema kutakuwa na Makongamono ya uwajibikaji, michezo na midahalo mbalimbali ambapo kutakuwa na viongozi mbalimbali ngazi za kiserikali ,na Bunge kuja kuchangia hiyo mijadala ikiwa na lengo la kuendeleza mahusiano mazuri na kuleta mabadiliko chanya ,”amesema

Naye Mkurugenzi mkazi CBM Tanzania Nesia Mahenge alisema kuwa Katika maonyesho hayo kutakuwa na Tuzo mbalimbali ambazo zitatolewa kwa kupitia hatua mbalimbali zitapendekezwa ambazo pia zitawashirikisha waandishi wa Habari ambao wamekuwa wakiandika Habari za Azaki na kuzitangaza.

“Tutakuwa na zawadi mbalimbali kwa kwa mashirika yaliyofanya kazi kwenye jamii Kuhusu mambo ya na Asasi za kiraia na tutawashirikisha vyombo vya habari katika mchango wao waliouleta ambao wametangaza Habari zetu kwa wingi au Mwandishi aliyejikita kutangaza habar za Azaki “amesema Mahenge

Kwa upande wake Shaki Shalaji ni mwakilishi Msajili ya Mashirika yasiyokuwa ya kiserikali NGO’s kutoka Wizara ya Afya maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto, alisema Katika Wizara Wana sera ya 2011 ya kuhakikisha wanaweka mazingira wezeshi ili waweze kufanya kazi kwa weledi .

Amesema kuwa mashiriki haya yatazingatia utaratibu wote ulioanishwa na Wizara ya Afya huku wakilindwa kwani mashiriki hayo yamekuwa yanafanya kazi kubwa na Serikali Kutoa elimu, kuweka vitakasa mikono na kuhamasisha Jamii kupata chanjo .

Awali akizungumza na vyombo vya habari Mkurugenzi wa Foundation for Civil Society Fransic Kiwanga amesema Kwenye maonyesho kutakuwa na wigo mpana na lengo mojawapo ni kusherekea yale waliyoyafanya kwa kipindi chote tangu kuanzishwa kwa maonyesho hayo mwaka 2018 huku kauli mbiu ikiwa ni “mchango wa Asasi za kiraia ni kujenga nchi”.

Pia amesema lengo lingine ni kuondoa mtazamo uliojengeka kwenye akili za watu kwamba mchango wa Azaki sio mkubwa sana na kutambua umuhumu wake kwani tangu wamefanya maonyesho kumekuwa na mwitikio mkubwa sana kwa jamii.

“Licha ya hayo lengo la maonyesho ya wiki ya Azaki ni Kuboresha mahusiano yaweze kujengeka vizur Kati ya Sekta mbalimbali na Jamii kwa ujumla hivyo niwasihi Watanzania kuja kwenye maonyesho hayo ambapo Kutakuwa na burudani za tamaduni mbalimbali na kutambua mchango wa kila mtu,”amesema Kiwanga.