September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ramani ya Mkoa wa Simiyu

Watu 120 wawekwa karantini Simiyu

Na Bahati Sonda, Simiyu

WAGENI 120 waliowasili mkoani Simiyu wakitoka nje ya nchi wamewekwa karantini kwenye mabweni ya shule za sekondari, huku 18 wakiruhusiwa baada ya kumaliza siku 14 za uangalizi na kubainika hawana maambukizi ya virusi vya corona.

Hatua hiyo ni utekelezaji wa agizo la Serikali lililotolewa Machi 23,2020 la kutaka watu wote wanaotoka nje ya nchi kuwekwa karantini ikiwa ni sehemu ya mkakakati wa kupambana na corona.

Idadi hiyo ilitolewa jana na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt. Festo Dugange, wakati wa upuliziaji dawa kwenye mabasi ya mikoani lililoongoza na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Athony Mtaka.

Alisema watu waliopo karantini wanapewa elimu ya virusi vya corona kuhusiana na namna ya kujikinga ili watakaporudi kwenye maeneo yao wawe mabalozi kwa wengine.

Akizungumza mara baada ya zoezi hilo, Mtaka alisema watu wengi waliopo kwenye karantini wameenda kwa hiari yao bila kutumia nguvu yoyote.

“Watu hawa hawajatafutwa na polisi tunao watu wanaotoka safari za mbalimbali na kuja kuomba wenyewe watengwe na wengine familia zao zinaleta taarifa zenyewe kuwa tuna mgeni wa aina fulani, tunaomba ajitenge na watu wamekuwa na uelewa wa kutosha, kwani zinapoona mgeni zinatoa taarifa kwenye mamlaka husika nayo inachukua hatua,”alisema Mtaka

Kamanda wa Mkoa wa Simiyu, Henry Mwaibambe aliwataka wananchi wa mkoa huo kufuata maelekezo yaliyotolewa na Serikali na kwamba Polisi hawatasita kuchukua hatua za kisheria kwa mtu yeyote ambaye atakiuka au kushindwa kufuata maelekezo.