May 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TMA yatoa ufafanuzi juu ya Mwaga wa ajabu angani

Na Penina Malundo

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa ufafanuzi juu ya hali iliyoonekana juzi ya angani ya rangi nyekundu au rangi ya Chungwa na kusema kuwa ni hali ya kawaida ambayo hutokea wakati jua linapozama au kuchomoza.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya Habari Jana Jijini Dar es Salaam, imesema katika mazingira yenye kuwa na hali ya hewa kama vile mawingu, matone madogo madogo ya maji na barafu katika anga mara mvua inapokatika na jua linapokuwa katika upande tofauti na eneo la mvua inaponyesha hali inayosababishwa kutawanywa kwa miale ya mwanga wa jua.

Imesema, kutokana na ukubwa wa matone ya maji katika wingu na chembechembe za vumbi katika anga, sehemu ya miale ya jua inayotawanywa zaidi katika mazingira yanayofanya kuwa na mawimbi ya miale ya jua inayohusiana na rangi nyekundu au chungwa.

Kutokana na hali hiyo haina tofauti sana na namna Upinde wa Mvua unavyojitokeza angani, isipokuwa upinde mvua unakuwa na rangi zote saba za spectrum ya mwanga.

“Mabadiliko hayo ya hali ya anga hayana madhara yeyote katika hali iliyozoeleka mara nyingi, anga huonekana kuwa rangi ya bluu kutokana na kutawanywa kwa mawimbi ya miale ya jua kunako fanywa na gesi ya Nitrojeni na Oksijeni ambazo ndizo hufanya sehemu kubwa ya gesi katika hewa,” imesema sehemu ya Taarifa hiyo

Pia hali hiyo inatokana na molekuli za gesi hizo kuwa ni ndogo sana hivyo hutawanya sehemu ya mawimbi madogo zaidi ya miale ya jua iliyo katika rangi ya blue katika spectrum ya mwanga.