March 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watoto wawili waokotwa kwenye Majaruba Mwanza

Na Mwandishi Wetu, Mwanza

WATOTO wa wawili wameokotwa wametupwa kwenye shamba la mpunga(majaruba) wakiwa bado hai, lakini katika mazingira magumu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro, aliwaambia waandishi wa habari mkoani hapa kuwa watoto hao wa jinsia ya kiume na kike waliokotwa Aprili 27, mwaka huu

Amesema tukio hilo lilitokea saa 11 alfajiri katika Mtaa wa Mtakuja Kata ya Nyamhongolo Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza, ambapo watoto wawili wa kwanza jinsia ya kiume anayekadiriwa kuwa na mwaka mmoja akiwa amevalia fulana ya rangi ya bluu na pili jinsia ya kike anayekadiriwa kuwa na umri wa miezi mitatu akiwa amevalishwa nguo moja
mwili wote rangi nyeupe walikutwa wametupwa kwenye shamba la mpunga.

RPC Muliro amesema; “Watoto hao walikutwa wakiwa wametupwa kwenye shamba la mpunga/majarubani wakiwa katika mazingira magumu, lakini wakiwa hai.”

Amesema kitendo cha kuwatupa watoto hao ni miongoni mwa makosa makubwa ya kikatili dhidi ya watoto na hakivumiliki. Alisema watu wote waliohusika watasakwa popote walipo na watakamatwa na kufikishwa mahakamani.

RPC Muliro amesema watoto hao wamepelekwa Hospitali ya Rufaa ya Bugando kwa ajili ya matibabu na hali zao zinaendelea vizuri.