April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watoto wahukumu madereva katika mahakama ya watoto

Na David John TimesMajira Oniline, Dar Es Salaam

KAMANDA wa Polisi kikosi cha Usalama Barabarani Willbroad Mutafungwa amesema uwepo wa Mahakama  ya watoto ya ukiukwaji wa makosa ya Barabarani unasaidia kwa kiwango kikubwa kupunga ajali zisizokuwa za lazima.

Kamanda wa Jeshi la Polisi ,Kikosi cha Usalama Barabarani Wilbroad Mutafungwa ( wa kwanza kushoto waliokaa) akiwa na wanafunzi wa Shule ya Msingi Olimpio jijini Dar es Salaam wakati wanafunzi hao wakisikiliza kesi za madereva waliovunja sheria za Usalama Barabarani kupitia programu ya Makakama ya Watoto yenye lengo la kutoa elimu ya usalama barabarani.Aliyekaa mbele ya Kamanda Mutafungwa na wanafunzi hao ni mmoja wa madereva ambaye alikamatwa na askari wa Usalama Barabarani kwa kosa la kutosimama kwenye kivuko cha waenda kwa miguu kilichopo eneo la shule hiyo juzi.

Mutafungwa amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati akishuhudia uendeshwaji wa mahakama hiyo na kusomewa mashtaka pamoja na kupewa hukumu kwa baadhi ya madereva waliokuwa wakifanya makosa na kufikishwa kwenye chumba maalumu katika shule ya msingi Olimpio iliyopo Upanga  wilayani Ilala.

Amesema kuwa  Mahakama hiyo inaleta msaada mkubwa katika jamiii na hasa katika kuondosha au kupunguza uwepo wa Makosa ya barabarani kwa madereva ambao wanashindwa kufuata sheria za barabarani zilizowekwa na mamlaka husika.

“leo nimekuja kushudia hapa mimi Mwenyewe uendeshwaji wa Mahakama hii ya watoto  kwakweli watoto hawa wanauwezo mkubwa sana embu fikiria  wanakuuliza maswali mtu mzima na unatoa ahadi na  kiyapo cha  kutorudia makosa jambo hili ni zuri na sis kama Jeshi la Polisi kikosi cha usalama barabarani tutaendelea kutoa ushirikishirikiano mkubwa kwa shirika hili la Amendi.”amesema Kamanda Mutafungwa.

Wanafunzi wa Shule ya Msingi Olimpio mkoani Dar es Salaam ambao wapo kwenye Programu ya Makakama ya Watoto wakiwa makini kuangalia mmoja wa madereva akiandika kiapo cha kutorudia kuvunja Sheria ya Usalama Barabarani baada ya kukiri mbele ya Wanafunzi hao kuvunja sheria hizo baada ya kutosimama kwenye kivuko cha waenda kwa miguu kilichopo nje ya shule hiyo .Wa kwanza kushoto ni Kamanda wa Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Wilbroad Mutafungwa akifuatilia uendeshaji kesi uliokuwa unafanywa na wanafunzi hao wakati Makakama ya Watoto ikiendelea.

Pia Kamanda Mutafungwa alilipongeza shirika la Amendi kwa kujitoa kwao na kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha wanatumia Mahakama hiyo ya watoto kutoa elimu.kwa madereva nchini nzima hususani kwenye maene ya mashuleni.

Niwapongeze  sana Amendi wanafanya kazi kubwa sana katika kuhakikisha wanatoa elimu hii kupitia watoto hawa na sisi tutaendelea kutoa kila ya aina ya ushirikiano kwao.nakuyataka Mashirika mengine kujitokeza ili kuhakikisha ajali za barabarani zinamalizika”amesema .

Akizungumzia kuhusu Ajali za barabrani amesema kuwa kwa asilimia kuwa ajali zimepungua sana na wataendelea kutoa elimu ya usalama barabarani ili kuona mwisho wa siku ajali zinamalizwa kwa asilimia kubwa kama si kutokomezwa kabisa.

Kwaupande wake mkurugenzi mtendaji wa shirika la Amendi Simon Kalolo amesema kuwa wao kama wadau wa usalama barabarani kwakushirikiana na Jeshi la Polisi kitengo cha usalama barabarani kazi kubwa wanayofanya nikutoa elimu ya usalama barabarani.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Wilbroad Mutafungwa (kulia) akijadiliana jambo na Mkurugenzi wa Shirika la Amend Tanzania Simon Kalolo( katikati) na Meneja Programu wa Shirika hilo Neema Swai( kushoto) baada ya kumalizika kwa Mahakama ya Watoto iliyokuwa inasikiliza kesi ya madereva waliovunja sheria za Usalama Barabarani.Mahakama hiyo imeendeshwa na wanafunzi wa Shule ya Msingi Olimpio mkoani Dar es Salaam.

Amesema kuwa katika kuhakikisha wanapunguza ajali hizo za usalama wa barabarani hivi sasa wamekuja na Mahakama ya watoto mashuleni ambayo kazi yake kubwa itakuwa ni kuwahukumu madereva ambao wanavunja sheria za alama za usalama barabarani na kusababisha ajali zisizo za lazima.

Amefafanua kuwa wamekuja na Mahakama hiyo ikiwa ni sehemu ya ubunifu kwa lengo la kufikisha meseji ya moja kwa moja  kwa watumiaji wa vyombo vya moto kwani anaamini watumiaji wengi wanapohojiwa na watoto wadogo kwa makosa ambayo wanayafanya watajisikia vibaya na ni rahisi kubadilika.

Wanafunzi wa Shule ya Msingi Olimpio mkoani Dar es Salaam ambao waliokuwa wakiendesha kesi katika Mahakama ya Watoto kwa kusikiliza na kutoa hukumu kwa madereva waliovunja sheria za Usalama Barabarani katika eneo la shule yao.

” Huu ni ubunifu tu ambao sisi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kitengo cha usalama barabarani tumeufanya na kwakweli Mahakama hiii imekuwa ikifanya vizuri sana na hadi sasa tumeshazifkkia shule karibu nane na lengo nikuona tunatekeleza mradi huu kwa nchi nzima.”amesema Kalolo

Ameongeza kuwa watoto hao wamekuwa wabunifu na kwakweli wengi wao ukiwauliza wanasema wanatamani waje kuwa Mahakimu na hiyo ina tokana na uhodari na ujasili wanaouonyesha katika kuuliza maswali kwa madereva ambao wanafanya makosa hayo.

Nao watoto hao kwa pamoja wamesema madereva wanatakiwa wawe makini na wasiwachukulie poa kwa sababu wao ni watoto wadogo kwani wakifanya makosa na kufikishwa mbele ya Mahakama yao wajuwe watakabiliana na maswali magumu na watapata hukumu na kula kiapo cha ahadi cha kutofanya tena makosa ambayo yanapelekea kusababisha ajali hususani kwa watembea kwa miguu (vivuko)

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Wilbroad Mutafungwa (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na walimu wa Shule ya Msingi Olimpio mkoani Dar es Salaam , Mkurugenzi wa Shirika la Amend Tanzania Simon Kalolo ( wa pili kushoto),maofisa wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani pamoja na wanafunzi wa Shule hiyo.
Kamanda wa Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Wilbroad Mutafungwa (katikati) akiwa na maofisa wa Jeshi hilo pamoja na Mkurugenzi wa Shirika la Amend Tanzania Simon Kalolo ( wa tatu Kushoto) na Meneja Programu Neema Swai(wakwanza kushoto).