September 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watanzania watakiwa kulinda, kuenzi mila

Na David John,TimesMajira Online. Njombe

MKUU wa Wilaya ya Iringa mjini, Richard Kasesela amewataka Watanzania kuendelea kulinda na kuenzi mila na desturi za kiafrika, kwani zimekuwa na msaada mkubwa katika jamii hususan Tanzania.

Amesema hivi sasa Watanzania wamekuwa na changamoto ya kudharau mila, desturi na ya maduni za Kiafrika jambo ambalo wakati mwingine inaleta changamoto kubwa, hivyo ni vyema tamaduni zikaenziwa kwani ndio asili ya Uafrika.

Kasesela ameyasema hayo juzi mjini hapa akiwa katika ziara ya kutembelea msitu wa Nyumba Nitu uliopo mkoani hapa, ambapo msitu huo ulikuwa unatumiwa na Machifu wa kabila la Wabena kufanya ibada za mila.

Pia amesema katika eneo la msitu huo, pawekwe mazingira rafiki yatakayorahisisha watu kufika katika eneo na kufanya utalii, ambao utasababisha hata kupata kipato lakini kuwawezesha watalii kuona mambo ya kale, ambayo yalikuwa yanatumiwa na wazee pamoja na Machifu.

Wakati huo huo Mkuu huyo wa Wilaya, ameitaka jamii ya kabila la Wabena kuacha kuwapa watoto pombe ya ulanzi, kwani kufanya hivyo kunasababisha udumavu wa akili.