September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watanzania wafanyabiashara na wawekezaji watakiwa kuchangamkia fursa

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Watanzania wafanyabiashara na wawekezaji wametakiwa kuchangamkia fursa za wageni kutoka nje wanaokuja kuwekeza nchini ili washirikiane na kupelekea kupata mtaji na teknolojia.

Wito huo ulitolewa jana na Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Peofesa. Kitila Mkumbo wakati akizungumza katika kongamano la uwekezaji na biashara baina ya Tanzania na China ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 60 ya mahusiano ya kidiplomasia kati ya Tanzania na China  lililoandaliwa na TIC, TPSF na TanTrade ambapo ujumbe wa makampuni 100 kutoka china wameshiriki kwaajili ya kutafuta fursa za uwekezaji nchini Tanzania.

“Tanzania na China zina mahusiano ya miaka mingi ambapo Rais wao alipochaguliwa nchi ya kwanza kutembelea Afrika alichagua Tanzania na marais wetu wote sita katika nchi hii wameshatembelea china , hivyo mahusiano haya yanatuonyesha kwamba China wanaweza wakawekeza hapa kwa uzuri lakini muhimu ni kwamba tayari tuna makampuni mengi ya kichina yamewekeza hapa” 



Aidha alisema bidhaa ambazo zinazalishwa hapa Tanzania na makampuni ya kichina na makampuni mengine ambazo zinaingia kutoka nje wao kama serikali wameweka mazingira kuhakikisha kwamba zinakua na ubora uliokidhi ili wasiathirike kwa namna yoyote.

“China kwa sasa Duniani ndiyo inayoongoza katika eneo la uzalishaji na bidhaa nyingi ambazo zinakuja nchini zinatoka nchini hivyo kama nchi vipo viwango vya kisheria vya  bidhaa ambavyo wanaviangalia “

Prof. Mkumbo alisema kupitia Dira ya 2050 moja ya eneo kubwa ambalo wataliangalia itakuwa ni mageuzi ya kiuchumi .

“Mageuzi ya kiuchumi
Lazima uwekezaji uongezeke, lazima tuende kwenye uchumi wa viwanda na makampuni haya ambayo yanatoka nje kuja kuwekeza nchini ni eneo muhimu, pia lazima tuvutie FDI kwa maana ya mtaji kutoka nje kwa kukaribisha makampuni kutoka nje na kuvutia teknolojia katika mataifa yaliyoendelea ikiweno Taifa la chini lakini pia suala la mtaji, bila mtaji huwezi kukuza uchuni”



Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kituo cha uwekezaji Tanzania (TIC),  Gilead Teri alisema wawekezaji ambao wametoka china kuja nchini Tanzania wamekuja kutafuta fursa katika sekta mbalimbali ikiweno Nishati, viwanda n.k

“Wawekezaji hao wamekuja kwenye sekta kadhaa ikiwemo nishati, wanaangalia uzalishaji wa vifaa pamoja na bidhaa zinazofanikisha umeme wa jua, tunao wawekezaji kwenye sekta ya viwanda ambao wamekuja kwenye viwanda vya bidhaa za ujenzi, usimikaji chakula , kwenye sekta ya ujenzi na madini, Katika maeneo haya watanzania pia tumewaalika ili waweze kufahamiana washirikiane waanzishe makampuni pamoja na wafanye uwekezaji kwa pamoja”

Alisema China ni moja ya nchi ambazo zina mitaji mikubwa Duniani ambapo wao kama TIC wanawatambua na kuwapa kipaumbele kama wawekezaji muhimu nchini ambao wakishirikiana na watanzania kutakuwepo na matokeo makubwa sana nchini.


Naye Kaimu Mkurugenzi Idara ya ukuzaji wa Biashara kutoka TanTrade, Tito Nombwa alisema wamekuwa pamoja na TIC kuhakikisha kwamba wanafanikisha kongamano hilo lakini pia wanakuza biashara kwa kuhakikisha wawekezaji wanaokuja nchini baada ya kuzalisha wanapata masoko.


Wawekezaji wa Tanzania walioshiriki kongamano hilo walisema ujio wa wawekezaji hao imekua chachu kwao kwani wamebadirishana uzoefu ikiwemo matumizi ya teknolojia.