May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wasimamizi wa vituo vya kupiga kura Nzega waonywa kutoingiza maelezo binafsi

Na Tiganya Vincent, TimesMajira Online,Tabora

WASIMAMIZI wa Vituo vya Uchaguzi wameonywa kutoingiza maelekezo yao binafsi wakati wa zoezi la upigaji kura bali wametakiwa kuzingatia Sheria ,Kaununi na miongozo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC) ili uchaguzi uweze kufanyika kwa amani na ufanisi mkubwa.

Wasimamizi Wakuu na Wasaidizi wa Vituo vya Uchaguzi wa Jimbo la Nzega Mjini wakiapa jana wakati wa wakati wa mafunzo ya maelekezo kwao kuhusu Sheria , Kanuni , Taratibu zinazosimamia zoezi la Kupigia Kura

Kauli hiyo imetolewa na Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Nzega Mjini Philemon Magesa wakati akifungua mafunzo ya maelekezo kwa Wasimamizi Wakuu na Wasimmizi wasaidizi wa Vituo vya Kupigia Kura.

Amesema wamepewa dhamana kubwa kwa hiyo wanatakiwa kuwa na uadilifu na kutopendelea wakati utekelezaji majukumu waliyopewa ili kuhakikisha kuwa uchaguzi unafanyika bila kusababisha migogoro yoyote katika maeneo yao.

“Msifanye vitendo kinyume na maelekezo ambayo mmepewa na Tume …bali mnatakiwa kuzingatia Sheria, kanuni , miongozo na maelekezo ya Tume” amesisitiza.

Amesema kwa kuzingatia Sheria itasaidia kuufanya uchaguzi kuwa mzuri, wenye ufanisi na hivyo kuondoa kabisa malalamiko au vurugu wakati wote wa mchakato wa uchaguzi.

Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Nzega Mjini Philemon Magesa wakati akifungua jana mafunzo ya maelekezo kwa Wasimamizi Wakuu na Wasimamizi wasaidizi wa Vituo vya Kupigia Kura.

Magesa ameongeza kuwa ni muhimu wakati wa zoezi la upigaji kura Msimamizi wa Kituo akahakikisha kunakuwepo na utulivu na usalama wa wakati wote wa upigaji kura.

Amesema endapo wataona kuwepo kwa vishiria vya kuhatarisha usalama wasisite kutoa taarifa kwa Msimamizi Msaidizi Ngazi ya Kata ama Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo ili hatua zichukuliwe mapema.

Aidha Magesa aliongeza kuwa katika utekelezaji wa majukumu yao ni muhimu wakashirikiana na Mawakala wa vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi katika masuala ambayo wanastahili kushirikishwa ili kurahisisha utendaji kazi.

Msimamzi huyo wa Uchaguzi Jimbo la Nzega Mjini alisema ni Msimamizi wa Kituo cha Kupigia Kura pekee ndiye anayeruhusiwa kuwa na simu ndani ya Kituo.

Katika hatua nyingine Magesa amesema maandalizi ya upigaji kura katika Jimbo hilo kwa ngazi ya Rais, Mbunge na Madiwani limekamilika na vifaa vyote muhimu vipo tayari.