May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wananchi watakiwa kutunza miradi

Na Mwandishi wetu, Timesmajira Online

Mkuu wa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Kasilda Mgeni amewataka wananchi kuhakikisha kila mmoja kwenye eneo lake anashiriki kikamirifu kuilinda na kuitunza miradi yote iliyozinduliwa na Mwenge wa Uhuru 2024 ili iendelee kuwa na manufaa kwa vizazi vya sasa na vijavyo kama ilivyokusudiwa katika utekelezaji wake.

Mwenge wa Uhuru 2024 umepokelewa Wilayani humo mwaka huu na kuzindua miradi nane ya maendeleo katika sekta ya barabara, elimu, afya, maji, mazingira, vijana na makundi maalum, yenye thamani ya zaidi ya bilioni 3.6 fedha mabzo zimetokana na michango ya wananchi, Halmashauri na Serikali kuu.

“Nitumie nafasi hii kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ndani ya miaka mitatu ya uongozi wake sisi Wialaya ya Same tumepokea fedha za maendeleo zaidi ya bilioni 54 ambazo zimetumika katika utekelezaji wa miradi mbali mbali ikiwemo iliyozinduliwa na Mwenge wa Uhuru 2024, ni jukumu letu sasa wana Same kuhakikisha tunailinda na kuitunza miradi hiyo ili iendelee kuwa na manufaa kwa vizazi vyetu vya sasa lakini na vijavyo pia kama ilivyokusudiwa katika utekelezaji wake.”

Aidha amewashukuru wananchi wa Same lakini pia vijana wa hamasa ya Mwenge kwa kuitikia wito kujitokeza kwa wingi kushiriki kikamirifu kupokea, kukimbiza pia kwenye mkesha wa Mwenge wa Uhuru, pamoja na uzalendo wa hali ya juu na kazi nzuri waliyoifanya na kusisitiza kuwa Serikali inatambua sana mchango wa vijana wazalendo kwenye ujenzi wa Taifa, sasa ni wakati wao kujikita kwenye shughuli za uzalishaji ili waweze kujitegemea kwani Serikali inaendelea kutengenenza fursa nyingi za Maendeleo kwa vijana.

Vile vile amesisitiza kuendelea kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa 2024 Godfrey Mzava, kwanza wa kutunza mazingira kwa kuendele kupanda miti kwenye maeneo yetu, kuungana kwa pamoja kupinga rushwa ikizingatiwa tunaelekea kwenye Uchaguzi wa Serikali za mitaa, lakini pia kuacha kuendeleza kilimo cha madawa ya kurevya kwani sote tunatambua madhara yake kwa vijana wetu ambao ndiyo waathirika namba moja.”