March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wananchi Laela waipa ‘Heko’ CCM wasema “Oktoba tunatiki”

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online

BAADHI ya wananchi wa mji mdogo wa Laela, uliopo Halmashauri ya Sumbawanga Vijijini, wamekipongeza Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa maendeleo kiliyowaletea katika kipindi cha miaka minne chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Miongoni mwa miradi ya maendeleo iliyotajwa na wananchi hao ni pamoja na ujenzi wa shule za kutosha, vituo vya afya, miundombinu ya barabara pamoja na kuwakwamua vijana kiuchumi kupitia mikopo ya Halmashauri.

Wakizungumza na Mwandishi wa Timesmajira Online, katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa Laela A, Wilaya ya Sumbawanga Vijijini mkoani Rukwa, ikiwa ni muendelezo wa mikutano ya kampeni ya Mgombea Mwenza wa kiti cha Urais kwa tiketi CCM, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi kuelekea uchaguzi mkuu unatarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.

Prisca Mengo mkazi wa kijiji cha Uleche,amesema,Serikali imetuletea maendeleo katika Sekta mbalimbali ikiwemo upande wa kilimo, elimu na afya.

“Mfano hivi sasa tuna madarasa ya kutosha katika kila eneo, lakini tuna changamoto ndogo katika Kijiji cha Kalambanzite kwenye eneo la afya tuna upungufu wa madaktari na ukosefu wa wodi za kupumzishia wagonjwa”, amesema Prica.

Kwa upande wake, Katibu wa Vijana ngazi ya Kata, James Kachenje, amesema kutokana na mambo mengi yaliyofanywa na Serikali hawatuna budi kusema kuwa Oktoba wanatiki kwa CCM.

“CCM imegusa kila rika, hususani hata kwetu sisi vijana kwani mbali na maendeleo ya miundombinu pia ni wanufaika wa mikopo ya halmashauri, jambo linalotusaidia kuturahisishia maisha yetu,”amesema Kachenje.

Nae Alkado Thomas mkazi wa Laela, amesema hana shaka na wagombea walioteuliwa na chama kugombea katika nafasi za uongozi kuanzia ngazi ya chini hadi juu hivyo wanaenda kukipa ushindi chama hicho.

Aidha, ameiomba Serikali kupitia CCM endapo ikipata ridhaa, kuboresha upatikanaji wa pembejeo kwa wakati na uwepo wa soko la mazao hususani zao la mahindi.