May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wakulima wa kahawa washauriwa

Na Zena Mohamed,TimesMajira Online

IMEELEZWA kuwa  miongoni mwa changamoto zinazoikabili sekta ya kahawa ni pamoja na tija ndogo,uzalishaji mdogo,kuyumba kwa bei katika soko la Taifa,ukosefu wa mitaji kwa wakulima na hivyo kushindwa kukopesheka kwenye taasisi za fedha mambo ambayo yanasababisha kilimo cha kahawa kuonekana kuwa hakilipi na kuwataka kuzalisha kwa tija.

Kauli hiyo imetolewa jijini hapa leo na Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Omary Mgumba wakati akifungua kongamano la 11 la wadau wa kahawa kutoka mikoa mbalimbali nchini.

Amesema, uzalishaji wa kahawa siyo mzuri  hivyo kongamano hilo litasaidia kuondokana na changamoto hiyo kwani limelenga zaidi kujifunza shughuli za maendeleo ya sekta  ya kahawa zinazotekelezwa katika maeneo mengine.

“Mazao haya ya kimkakati yanatakiwa kubadilika ,kukua kuweza kutoa mchango katika jitiahada za serikali za kutatua tatizo la ajira ,kuchangia katika ukuaji wa uchumi,ujenzi wa viwanda,kuongeza vifaa vya wakulima na kukuza uchumi wa wakulima”amesema Mgumba.

Mgumba amesema, zao la kahawa ni moja ya mazao ya kimkakati yaliyochaguliwa na serikali hivyo yanatakiwa kubadilika,kukua ili kuweza kutoa mchango katika jitihada hizo ikiwemo kutatua tatizo la ajira.

Pia amewataka wadau hao wa kahawa kuhakikisha Sekta ya Kahawa inabadilika kwa kuongeza ufanisi katika uzalishaji ili kupata soko la uhakika ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Prof. Aurelia Kamuzora amezungumzia umuhimu wa zao hilo katika maisha yake kwani limemsaidia kwa kiasi kikubwa kumfikisha hapo alipo leo. ‘’Mimi nina historia na zao hili, kwani limenisomesha na kunifikisha katika hatua niliyopo sasa,’’amesema Kamuzora.