April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wakulima Tunduru wauza ufuta tani 282,477

Na Steven Augustino,Timesmajira Online, Tunduru

JUMLA ya tani 282,477 za ufuta zilizowekwa sokoni kupitia mnada wa nne, zimeuzwa na wakulima kwa bei ya sh. 2,322 kwa kilo moja na kuingiza kisasi cha sh. 655,911,594 kwenye mzunguko wa fedha wilayani hapa.

Katika mnada huo uliofanyika katika Kijiji cha Marumba Kata ya Marumba wilayani hapa, jumla ya wanunuzi wanne na kutoa bei tofauti ambapo baada ya uchambuzi, wakulima waliridhika kutoa ufuta wao kwa mteja aliyeomba kununua kwa bei ya sh. 2,322, huku katika mnada huo kukiwa na kampuni ambayo iliomba kununua ufuta huo kwa bei ya sh. 1,935.

Akitoa taarifa za mnada wa tatu uliofanyika Tarafa ya Lukumbuke Ofisa Ushirika Wilaya ya Tunduru, George Bisani amesema jumla ya tani 429,947 ziliuzwa kwa bei ya sh. 2,280 na kuingiza pato la sh. 980,540,114 katika wilaya yao.

Amesema mashindano ya wazi kwa wanunuzi kupitia mfumo unaendelea kuonesha manufaa makubwa kwa wakulima ikiwemo kuingiza fedha nyingi kwenye mzunguko wa wilaya pamoja na kuongezeka kwa bei ya mazao.

Bisani amesema hadi mnada wa nne tayari wakulima wa ufuta, wamekwishaongeza sh. 3,600,796,928 kwenye mzunguko wa fedha ndani ya wilaya, baada ya kuuza tani 1,608,732 za ufuta wao msimu huu.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Meneja wa Chama cha ushirika Wilaya ya Tunduru (TAMCU) Imani kalembo, Yasin Masiano amesema tayari wameanza kuwalipa wakulima waliouza ufuta wao katika mnada wa kwanza na wa pili.

Katika taarifa hiyo, Masiano amewahakikishia wakulima hao kuwa TAMCU kupiatia Vyama vya Msingi Amcos za wilaya hiyo, wamejipanga kuhakikisha wakulima wote wanalipwa stahiki zao muda mfupi baada ya wanunuzi kuingiza malipo yao.

Awali akifungua mkutano wa mnada huo Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Wilaya ya Tunduru (TAMCU), Mussa Manjaule amewataka wanunuzi kuongeza bei katika minada ijayo, ili kumuinua mkulima na kuwafanya waongeze juhudi za mkulima mazao mengi zaidi katika msimu ujao.