September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wakazi Siha wajitolea kujenga shule ya msingi

Na Allan Vicent,TimesMajira Online. Siha

WAKAZI wa Kijiji cha Ngarenairobi wilayani Siha Mkoa wa Kilimanjaro kwa kushirikiana na serikali, wamejitolea kujenga shule mpya ya msingi katika kijiji hicho, ili kumalizia kero ya muda mrefu kwa watoto wao kutembea umbali mrefu wa zaidi ya kilomita tatu kwenda shule iliyoko kijiji jirani.

Baadhi ya wananchi hao, waliliambia Majira kuwa wamelazimika kuanza ujenzi wa shule hiyo kwa kushirikiana na serikali, kutokana na umbali mrefu na msongamano mkubwa wa watoto katika Shule ya Msingi Mwangaza iliyoko Kijiji cha Mwangaza wilayani hapa ambako ndiko wanakosomea.

Wakizungumzia ujenzi huo wakazi wa kijiji hicho, Lameck Msonga na Aidan Maarifa walisema msongamano mkubwa wa watoto darasani, unasababisha hata matokeo ya watoto wao kutokuwa mazuri jambo ambalo limewasukuma kuchukua hatua ya makusudi ya kuunga mkono juhudi za serikali kwa kujitolea kujenga shule hiyo katika kijiji chao.

Waliongeza kuwa kwa sasa chumba kimoja wanakaa watoto kati ya 100 hadi 120 hali inayopelekea hata walimu kushindwa kuwafundisha ipasavyo kutokana na msongamano huo, hivyo wakabainisha kuwa wanataka kumaliza tatizo hilo ili watoto wao wasome vizuri na kuendelea na masomo ya sekondari.