May 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Afisa Masoko kutoka Jatu PLC, Ngorosho Winfrid akitoa elimu ya namna ya kununua hisa kupitia kampuni hiyo.

Waitwa Sabasaba kununua hisa kwa 500/-

Na David John, TimesMajira Online

WATANZANIA wameshauriwa kujitokeza kwenye viwanja vya maonyesho Sabasaba wilayani Temeke mkoani Dar es Salaam ili kuona fursa mbalimbali ambazo zinapatikana kupitia maonyesho ya 45 ya biashara ya kimataifa yaliyofunguliwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Profesa Kitila Mkumbo.

Rai hiyo imetolewa wilayani humo na Ngorosho Winfrid ambaye ni Afisa Masoko kutoka Kampuni ya Jatu PLC ambapo amesema kuna haja ya wananchi kutembelea maonyesho hayo ili kuona fursa zilizomo.

Amesema, wao kama Jatu PLC wapo kwenye viwanja hivyo vya kimataifa vya Mwalimu Nyerere maarufu kama Sabasaba kwa ajili ya kuwapa fursa ya kununua hisa Watanzania na kuwa sehemu ya kampuni hiyo.

“Sisi kama Jatu tupo kwenye viwanja hivi vya Mwalimu Nyerere Sabasaba na kubwa zaidi tumekuja na kauli mbiu yetu ya Buku tano inatosha ambapo fedha hiyo itamwezesha mwananchi kununua hisa,”amesema Ngorosho.

Na kuongeza kuwa, “Ili kuweza kupata fursa ya kupata hisa Jatu inatakiwa kufika kwenye banda lao ukiwa na kitambulisho cha NIDA na shilingi 5,000 mkononi itakufanya kununua hisa ambapo hisa moja ni shilingi 500,”amesema.

Amefafanua kuwa, wapo katika hatua za mwisho kwani kampeni hiyo ya buku tano inatosha inatamatika mwezi Julai, mwaka huu hivyo ni vema kama wananchi wangechangamka katika siku hizi zilizobakia.

Ngorosho ambaye ni Afisa Masoko ameongeza kuwa, Jatu PLC ni kampuni ya kitanzania ambayo mwanzilishi wake ni mtanzania na amedhamiria kufanya mageuzi katika sekta ya kilimo.

Amesema, Jatu licha ya mambo ya hisa, lakini imejikita kwenye kilimo ambapo wanafanya kilimo karibu maeneo mbalimbali hapa nchini, lakini sio kilimo tu hadi masoko wanayo ndani na nje ya nchi.