May 10, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wahitimu wa vyuo vikuu watakiwa kutumia elimu yao kujiajiri

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Wito umetolewa kwa wahitimu wa vyuo vikuu katika kozi mbalimbali nchini, kutumia elimu walioipata kwa ajili ya kujiajiri ili waweze kujiletea maendeleo binafsi na taifa kwa ujumla.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Yuhoma Educational Limited Yusuph Yahaya,wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Mwanza kuelekea katika hafla ya usiku wa wadau wa habari Kanda ya Ziwa inayoandaliwa na Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Mwanza (MPC) itakayofanyika Mei 3,2022.

Yahaya ameeleza kuwa,dhima kubwa ya vyuo vikuu ni kuhakikisha inawajengea uwezo wanafunzi waweze kuishi katika mazingira mazuri ya maendeleo baada ya kuhitimu masomo yao katika ngazi mbalimbali za elimu.

Hivyo wahitimu wanapaswa kutumia elimu wanayoipata ili iweze kumsaidia katika kujenga uwezo wa kuishi kwa kujiajiri bila kusubilia kuajiriwa na serikali.

Ameeleza kuwa tangu kuanza uwekezaji mwaka 2015 amefanikiwa kuwapeleka nje ya nchi jumla ya wanafunzi 792 ambao wameweza kupata ajira serikalini na wengine wamejiajiri na wanaendelea vizuri.

“Wewe elimu ulionayo unatakiwa uitumie ili ikusaidie ujenge uwezo wa kuishi katika mazingira, tuna changamoto kubwa sana na wahitimu kwa sababu anasoma anakaa anasubilia serikali imuwezeshe ndio maana tumesema serikali inaweza kusaidia ukapata elimu tumia hiyo elimu ikusaidie katika kuishi katika mazingira ambayo unayo,”amesema Yahaya.

Pia ameeleza kuwa,njia nzuri ya kuweza kutatua tatizo ni kuelewa tatizo na kutatua ni hatua nyingine kuna wahitimu wanaelewa tatizo lakini hawajui namna ya kulitatua haina maana kuwa wote walio na PhD, Masters, na walio hitimu kuwa wote wanaweza kufanya vizuri.

Aidha Yahaya ametoa ushauri kwa jamii kuachana na habari kuwa Jiji la Mwanza limekuwa kitovu Bali watanzania na vijana wengi wasome ili waendane na sifa zinazohitajika katika kiwango cha kimataifa ili kuendana na soko la ajira.

Ili Wawe na teknolojia na wasifu mzuri ambao kesho na kesho kutwa watatumia na miradi mikubwa inayowekezwa nchini na Mkoani hapa iwe kipaumbele kwao na sifa kwao,vijana wasome ili wawe na sifa kwani hamna njia ya mkato,hata kama fursa itakuja chumbani kama hauna sifa hauna sifa tu ndio maana wanatafuta wataalamu kutoka nje.

“Sisi tumepata bahati Kanda ya Ziwa kweli sasa hivi miradi mingi ipo ya kimkakati changamoto iliopo ni wanafunzi kutokutaka kutafuta elimu na kubaki kulalamika, serikali itafanya sehemu yake lakini na wanafunzi wasome na kusoma kwenye tuna miradi tulionayo lazima tuende kwenye teknolojia uwezi kujenga daraja la busisi wakati elimu yako haitoshi lazima uwe na mkakati thabiti wa kuhakikisha kwa namna gani unaingia kwenye soko la ajira vinginevyo serikali italazimika kuleta watu kutoka nje wenye utaalamu kulingana na sifa zao watakuja tutawaona na mwisho wa siku tutaona miradi inaenda na sisi tutakosa ajira vinginevyo tutabaki kuwa vibarua tu,” amesema Yahaya.

Mbali na hayo pia ameiomba Serikali iwaamini na kuwasaidia vijana wenye ndoto za kwenda kusoma nje ya nchi pia wawawezeshe mikopo waweze kufikia malengo yao.

Mkurugenzi was Yuhoma Educational Limited Yusuph Yahaya akizungumza na Waandishi wa Habari mkoani hapa hawapo pichani katika kuelekea usiku wa wadau wa habari Kanda ya Ziwa.(Picha na Judith Ferdinand)