May 12, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wagonjwa 1148 wapatiwa matibabu ya kibingwa Igunga

Na Lubango Mleka, Igunga.

WAGONJWA 1148 kutoka Wilaya ya Igunga Mkoani Tabora na wilaya za jirani wamejitokeza kwa wingi kupimwa na kupatiwa matibabu na madaktari bingwa kutoka hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Dodoma na Nkinga kwa kushirikiana na madaktari wa hospitali ya wilaya ya Igunga.

Madaktari hao watatoa matibabu hayo katikab kambi hiyo ndani ya siku tano kuanzia Julai 24 hadi 28 Mwaka huu ambapo watatoa huduma za madaktari bingwa kwa magonjwa ya Macho, Maskio, Pua na Koo, Magonjwa ya kina mama na uzazi, upasuaji na magonjwa ya ndani.

Akisoma taarifa ya tathimini ya zoezi hilo kwa mgeni rasmi mbeye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Igunga Athumani Msabila, Mganga Mfawidhi hospitali ya wilaya ya Igunga Melchedes Magongo akiisoma kwa niaba ya Mganga mkuu wa wilaya Lucia Kafumu, amesema kuwa wananchi waliojitokeza kupima na kupatiwa matibabu ya madaktari bingwa walikuwa ni 1148 ambapo wanaume walikuwa ni 354 na wanawake ni 821.

” Magonjwa yaliyoongoza zaidi katika zoezi hili la matibabu ya kibingwa ni magonjwa ya kina mama na uzazi ambapo wagonjwa walikuwa ni 471, upasuaji walikuwa ni 307, magonjwa ya ndani jumla walikuwa 200 na magonjwa ya Macho ni 170, ambapo mafanikio katika zoezi hili wagonjwa wote waliojitokeza wamefanikiwa kupata matibabu ya kibingwa na wanaendelea vizuri, hivyo kutokana na wananchi kiujitokeza kwa wingi tunatarajia kutoabhuduma hizi mara tatu katika kila robo ya mwaka,” amesema Magongo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Igunga Athumani Msabila, ameutaka uongozi wa hospitali ya wilaya ya Igunga kuyafanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza ili kuendelea kutoa huduma bora za matibabu kwa wananchi, ikiwa ni pamoja na kuwapatia mafunzo wauguzi na waganga ili kuweza kutoa huduma za kibingwa muda wote.

“Nakupongeze Mganga mkuu na timu yako pamoja na madaktari hawa bingwa kwa kusogeza huduma hizi kwa ukaribu zaidi kwa wananchi, kwani sio wananchi wote wanaweza kwenda hospitali kubwa au za mikoani kupatiwa matibabu haya kutokana na vipato vyao kuwa vidogo, kuwasogezea huduma hizi ni kuwapatia faraja, changamoto zilizojitokeza tumezichukua na DMO atazifanyia kazi ili kuboresha zaidi ikiwa ni pamoja na kuandaa mafunzo na vifaa kwa wataalamu wetu,” amesema Msabila.

Amesema kusema kuwa ” Ili daktari bingwa aweze kutoa huduma ni lazima vifaa viwepo na dawa za kutosha, hata vilivyopo kama hakuna watu ambao wanaweza kuviendesha inakuwa ni changamoto, kwa hiyo Mganga mkuu ni vizuri kuangalia maeneo ambayo yanaitaji wataalamu wa kuendesha vifaa hivi kwa kuweka mkakati maalumu,”

Kwa upande wake Daktari bingwa wa Macho Rajabu Kisonga kutoka hospitali ya rufaa ya mkoa wa Dodoma ametoa shukarani kwa niaba ya jopo zima la madaktari bingwa, ambapo ameshukuru kwa mapokezi na ushirikiano walioupata toka kwa uongozi wa hospitali ya wilaya ya Igunga na kutoka kwa wagonjwa wote kwani wameweza kutoka huduma hiyo ya matibabu ya kibingwa kwa asilimia mia moja bila ya kuwepo na tatizo au malalamiko kutoka kwa wagonjwa.

“Niwapongeze uongozi na wananchi kwa mwitikio wao kwani wananchi wamejitokeza kwa wingi sana, tungependa kutoa ushauri wetu wanapokuja madaktari bingwa basi hospitali iandae madaktari na wauguzi hata wawili kila kituo kuja kujumuika na madaktari bingwa kwa lengo la kuongeza ujuzi zaidi na kutoa huduma hizi katika vituo vyao,” amesema Kisonga.

Huku baadhi ya wananchi waliojitokeza kupatiwa matibabu hayo, Happy Nyabukika, Francis Sambe, Evalista Mageru wakazi wa Igunga na Melkizedeki Kimaro mkazi wa kiomboi mkoani Singida wametoa wito kwa wananchi kujitokeza kucheki afya zao mara kwa mara na si kusubiri mpaka wasikie kuwa kuna madaktari bingwa kwani hospitali ya wilaya ya Igunga kwa sasa ina vifaa vya kisasa na wataalu ambao wanatoa tiba za matibabu hayo.

” Mimi niwasihii wananchi wenzangu kuacha mira potofu juu ya magonjwa kwa mfano magonjwa ya uvimbe, mtoto wa jicho namengine kuamini kuwa ni umelogwa na unaitaji kutibiwa kienyeji hilo si kweli, mimi nimefanyiwa upasuji wa jicho sasa hivi ninaona vizuri sana, kwa hiyo waje katika hospitali yetu wapate tiba,” alisema Sambe.

Naye Evalista Mageru ameiomba Serikali kuipatia hospitali ya Igunga madaktari bingwa ambao watasaidia wananchi wasio na uwezo wa kutafuta huduma hizo nje ya Igunga, kwani wananchi wamejitokeza ni wengi sana hivyo kufanya madaktari hawa bingwa kutumia muda wa ziada kutoa huduma hizo ambazo zimefanikiwa kwa kiasi kikubwa.