April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega akizungumza alipokutana na wadau wa mifugo pamoja na watendaji  walio karibu na shamba la kulishia mifugo la Shishiyu Holding Ground Wilayani Maswa wa  wakati wa ziara yake  wilayani humo alipotembelea na kukagua shamba la hilo. Picha na Judith Ferdinand

Wafugaji waikumbusha serikali ahadi ya eneo la kunenepesha mifugo

Judith Ferdinand, Maswa 

Wilaya ya Maswa, mkoani Simiyu imemkumbusha Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega, ombi la kupatiwa eneo katika pori la kituo cha Shishiyu Holding Ground kwa ajili ya mradi wa unenepeshaji na uzalishaji wa malisho ya mifugo.

Mkuu wa Wilaya ya Maswa Dkt.Seif Shekalaghe(mwenye miwani) akitoa taarifa kwa Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega katika ziara yake ya kikazi wilayani humo ya kutembelea na kukagua shamba la kulishia mifugo la Shishiyu Holding Ground. Picha na Judith Ferdinand

Akitoa taarifa kwa Naibu Waziri alipotembelea na kukagua shamba la mifugo la Shishiyu  Holding Ground, Mkuu wa Wilaya ya Maswa Dkt.Seif Shekalaghe amesema,Wilaya hiyo mwaka 2017 iliandaa andiko maalum la kuomba kukabidhiwa kituo hicho kwa ajili ya unenepeshaji na uzalishaji wa malisho ya mifugo.

“Nia hiyo bado ipo na maandiko ya kutafuta wafadhili kugharamia shughuli hizo yako katika hatua nzuri, hivyo kwa mara nyingine tunaomba kutengewa ekari 1,500 kati ya ekari 10,240 za eneo lote la Shishiyu Holding Ground,” amesema Dkt. Shekalaghe.

Amesema,wakishatengewa eneo hilo litatumika kama moja ya shamba darasa kwa wafugaji haswa unenepeshaji mifugo, uzalishaji, utunzaji wa malisho ya mifugo, uanzishaji wa kituo cha kiini tete na uzalishaji wa mbegu bora za mbuzi na kondoo. Kwa upande wa wafugaji anaomba wapatiwe vitalu vya kuchungia mifugo kwa masharti yatakayowekwa na wizara.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega, akizungumza katika kikao kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Maswa baada ya kusikiliza taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Wilaya hiyo Dkt.Seif Shekalaghe wakati wa ziara yake ya kutembelea na kukagua  shamba la mifugo la Shishiyu Holding Ground. Picha na Judith Ferdinand

Kwa sasa shughuli zinazofanyika katika kituo hicho ni wafugaji wa vijiji jirani kuchungia mifugo kwa kulipia ada ya malisho (grazing fee) ambayo ni shilingi 60 kwa mnyama mmoja kwa siku, ingawa vichaka vimepungua kwa kiasi kikubwa utoaji wa malisho ya mifugo huku miundombinu yake ikiwa chakavu ikiwemo nyumba za watumishi 6, majosho mawili,zizi la ng’ombe na bwawa moja lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita za ujazo milioni 2.4 kwa mwaka.

Hata hivyo kwa sasa  Wizara imeanza kufyeka vichaka kwa kutumia Gereza ya Malya  ambapo lengo ni kufyeka ekari 100 kufikia Mei 31 mwaka huu lakini mpaka sasa jumla ya ekari 70 zimeisha fyekwa na shughuli zinaendelea.