May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waajiri nchini watakiwa kulinda usalama, afya za wafanyakazi wao

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waajiri wote Nchini wametakiwa kuchukua hatua ya kuhakikisha wanalinda usalama na afya za wafanyakazi wao kama yalivyo matakwa ya Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi Namba 5 ya mwaka 2003.

Hayo aliyasema Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Prof. Joyce Lazaro Ndalichako ( MB) katika Kilele cha maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi ambapo kitaifa yamefanyika katika viwanja vya Tumbaku mkoani Morogoro ambapo Mwaka huu maadhimisho haya yamebeba kaulimbiu inayosema “Mazingira Salama na Afya ni Kanuni na Haki ya Msingi Mahali pa Kazi”

Akitoa salamu za Waajiri, Afisa Mtendaji Mkuu wa ATE, Suzanne Ndomba-Doran amesema kuwa ikiwa ATE ndiyo sauti ya Waajiri wote nchini kwa kushirikiana na wadau imekua mstari wa mbele kuwahimiza Waajiri kuzingatia na kutekeleza Matakwa ya Sheria ya Afya na Usalama mahala pa kazi ya mwaka 2003
ambapo sheria hiyo inamtaka Mwajiri kutengeneza mazingira yenye Afya na usalama mahali pa kazi na kutoa rai kwa wafanyakazi pia kufuata Kanuni na taratibu zilizowekwa mahala pa Kazi ili kuepesha migogoro isiyo ya lazima inayoweza kupelekea kushuka kwa ufanisi katika maeneo ya kazi.

“Mazingira salama ya kazi yanakayochochea uzalishaji na mahusiano mazuri. Kama mtakumbuka katika kuweka msisitizo katika jambo, Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Kazi wa 110, uliofanyika 2022 uliongeza kipengele cha usalama na afya kazini kuwa miongoni mwa mikataba ya Msingi katika Maeneo ya Kazi. Hii inamaanisha kwamba Usalama na Afya kazini ni jambo la msingi an la kuzingatia.”

Aidha Ndomba ameishukuru Serikali kwa jitihada kubwa katika kupunguza tozo za OSHA lakini pamoja na jitihada hizo, amesema wanaendelea kupendekeza kushushwa kwa gharama zinazotozwa mathalani tozo za upimaji wa afya za wafanyakazi na gharama za kufanya ukaguzi.

Naye Mtendaji Mkuu wa OSHA Khadija Mwenda akitoa salamu za ukaribisho amesema kuwa siku ya usalama na afya duniani ni siku muhimu ya Kimataifa ambayo Nchi zote wanachama wa Shirika la Kazi Duniani zilianza kuadhimisha siku kuanzia mwaka 2003

“lengo ni kuwawezesha wadau kupanua uelewa kuhusu ukubwa na madhara ya ajali na magojwa yatokanayo na kazi na kujenga uwezo katika kuweka sera na mikati ya kuzuia ajali na magonjwa kazini ili kufanya kazi zote ziwe za staha.”

Maadhimisho hayo yamehudhuriwa pia na Viongozi mbalimbali akiwemo Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Prof. Jamal Katindu, Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu ya Tanzania -Divisheni ya Kazi, Mhe. Dr. Yose Joseph Mlyambina, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ustawi na maendeleo ya jamii, Mhe. Fatma Hassan Tawfiq (MB), Mwakilishi wa Shirika la Kazi Duniani Bi. Getrude Sima, Viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Waajiri Nchini wakiongozwa na Rais wake, Bw. Tumaini Nyamhokya pamoja na viongozi mbalimbali na wakuu wa Taasisi Binafsi na Umma.

Pamoja na mambo mengine maadhimisho haya pia yameenda sambambamba na tukio la utoaji wa Tuzo kwa Waajiri waliofanya vizuri katika eneo la Afya na Usalama ambapo Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) wamekabidhiwa Tuzo ya Taasisi inayounganisha wadau wa maeneo ya kazi ili kuimarisha mifumo ya usalama na afya nchini