September 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vituo 77 vya Polisi vilivyoanzishwa kwa nguvu za wananchi kukamilishiwa

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online, Mwanza

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi · Daniel Baran Sillo amesema Serikali kupitia wizara hiyo itahakikisha inakamilisha ujenzi wa vituo vya Polisi 77 Nchi nzima vilivyoanzishwa kujengewa kwa nguvu za wananchi kwa mwaka wa fedha wa 2024/2025.

Sillo ametoa kauli hiyo Agosti 02, 2024 akiwa mkoani Mwanza wakati wa ziara yake ya kikazi ambapo amekagua ujenzi wa jengo la zahanati ya Polisi lililojengwa kwa ajili ya Idara ya Kinywa na Meno.

Pia amekagua ujenzi wa nyumba za kuishi Askari na kituo cha Polisi Nyegezi uliofikia hatua ya uezekaji.

Sanjari na hayo ameeleza kuwa serikali kupitia Wizara hiyo itajenga vituo vingine vya Polisi 12 kwenye Kata mbalimbali pamoja na kuboresha makazi ya nyumba za kuishi Askari wa Jeshi la Polisi kwa kutumia fedha za mfuko wa tuzo na tozo.