May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwenyekiti wa Chama United cha Democratic Party(UDP),John Cheo akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani)juu ya kumuunga mkono Rais John Magufuli katika Uchaguzi Mkuu.

UDP yamuunga Mkono Rais Magufuli Uchaguzi Mkuu

Yafungua dirisha la Uchukuaji fomu kwa Ubunge na Madiwani.

Na Penina Malundo, TimesMajira Online, Dar es Salaam

CHAMA cha United Democratic Party, (UDP) kimesema kipo tayari kumuunga mkono Rais John Magufuli endapo Chama chake kikimpitisha kuwa mgombea Urais katika Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba mwaka huu.

Pia kimesema Chama hicho kimefungua dirisha la wagombea Ubunge na Udiwani kuanza kuchukua fomu katika Ofisi zao.

Mwenyekiti wa Chama hicho,John Cheo amesema kipaumbele cha Rais Magufuli kuwainua wanyonge na kuleta maendeleo nchini ndio sababu iliyowafanya kuwaunga mkono.

“Namsifu Magufuli kuweka Mazingira mazuri hospitali karibu na wananchi,kutuimarishia miundombinu ya Barabara na Reli,” amesema na kuongeza kuwa

“Tumeamua kumuunga mkono Rais Magufuli endapo atapitishwa na Chama chake ila kama wasipompitisha tutatathimini kwanza ni nani tumpitishe alafu tutakuja na majibu kwa wananchi,” amesema

Pia amesema wamefungua dirisha la uchukuaji wa fomu leo na siku ya mwisho wa uchukuaji wa fomu hizo watatangaza kuendana na ratiba ya Tume ya Uchaguzi (NEC).

“Natoa Rai kwa wanachama wa UDP, kuja kuchukua fomu ili kuweza kupata nafasi ya kuingia katika baraza la maamuzi,” amesema