September 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

UDOM yafurahia ushindi,yaahidi kuja na tafiti za kusaidia jamii

Na Joyce Kasiki,Timesmajira ,Dar

CHUO Kikuu cha Dodoma (UDOM) kimesema kimekuwa kikifanya tafiti mbalimbali katika jamii ili kuja na bunifu ambazo zinatatua changamoto za jamii kutokana na tafiti husika.

Hayo yamesemwa jijini Dar Es Salaam na  Mkurugenzi wa Shahada za Awali UDOM, Dkt.Victor  Marealle mara baada ya Chuo hicho kuibuka mshindi wa kwanza kwa upande wa vyuo vya Elimu ya Juu kwenye maonesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara maarufu kama Sabasaba.

“Tuzo hii kwetu ni chachu kama Chuo kikuu cha Dodoma kuzidi kupambana zaidi, si tu kuboresha bidhaa ambazo tumezileta lakini kutatua matatizo kwa ujumla ambayo yanaizunguka nchi yetu na kuendeleza tafiti mbalimbali,” amesema.

Dkt.Marealle ambaye alikuwa msimamizi wa banda la ÙDOM kwenye maonesho hayo amesema kutokana na ushindi wa shughuli wanazozifanya ,wataendelea kufanya yafiti ambazo zitakuwa na tija katika kutatua changamoto zinazoizunguka jamii.

 “Tumefurahi kwa kupata ushindi namba moja kwa taasisi za Elimu ya Juu,ishindi huu utaendelea kuwa chachu katika utendaji wetu wa kazi zikowemo bunifu mbalimbali.” Amesema na kuongeza 

“UDOM  kimekuja na tafiti ambazo zinaenda kutatua changamoto katika jamii na siyo tafiti za kuweka makabatini au za kutumika nje ya nchi,

 “Kwa hiyo sisi tunakuja tofauti kidogo, tunakuja na tafiti ambazo tunashirikiana na tasnia hii moja kwa moja, tunatafiti kwanza mahitaji ya ndani  na nje halafu tunatengeneza programu ambazo zinakwenda kufiti tasnia inayotuzunguka,” amesema.

Amesema hata tafiti wanazozifanya zinaendana na matokeo ya moja kwa moja kwenye Sayansi, huku akisema katika maonesho hayo wamekuja na baadhi ya bunifu ambazo wamezigeuza na kuwa bidhaa zinazoingia sokoni.

“Sisi hatutaki machapisho yetu, kazi za watafiti wetu ziishie  kwenye mashelfu bali tunataka hizo kazi zikasaidie kutatua changamoto zinazoizunguka jamii hapa nchini.” Amesisitiza

Ametumia nafasi hiyo kuwakaribisha wanafunzi waliomaliza kidato cha sita ambao wanasifa stahiki za kujiunga na programu mbalimbali huku akisema UDOM wanashahada za awali hadi za uzamivu.

Aidha amesema moja ya  bunifu walizonazo ni bunifu ua satelaiti ambayo wapo katika mchakato wa kuirusha kwa ajili ya kusaidia kuboresha mawasiliano.