May 13, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Bado kuna changamoto kwa wenye ulemavu wa kusikia

Na Esther Macha, TimesMajira Online, Mbeya

MWENYEKITI wa Chama cha Viziwi Mkoa wa Mbeya , Tusa Mwalwega amesema kuwa kuhusu masuala ya wenye ulemavu na uongozi bado kuna changamoto nzito kuanzia ngazi ya serikali za mitaa mpaka taifa .

Mwalwega amesema hayo jana wakati akizungumza na gazeti hili mara baada ya kumaliza mkutano wa masuala ya uongozi kwa watu wenye ulemavu ,wanawake pamoja na vijana mkutano uliondaliwa na shirika la Elimisha.

Aidha mwenyekiti huyo amesema kuhusu nafasi za uongozi kwa watu wenye ulemavu wa kusikia bado kuna shida kubwa mfano mzuri Serikali za Mitaa watu wenye ulemavu wa kusikia wanaweza kuingia kwenye ofisi kuomba fomu na bado wakakataliwa .

“Mfano mzuri yupo mwanamke mmoja mlemavu wa kusikia aitwaye ,Lupi Mwaswanya aligombea ubunge Viti Maalum mwaka jana na kuongoza alipofika Dodoma changamoto ilikuwa wazi na wajanja walikuwa wengi ambapo walikuwa wanatoa rushwa na sisi walemavu habari ya rushwa hatujui wala mikakati ya kutoa rushwa,aligombea kwa mujibu wa haki lakini bahati mbaya akadondoshwa naamini hajakata tamaa na bado ataendelea kugombea tena “amesema Mwenyekiti huyo.

Akielezea zaidi kuhusu utendaji wa Rais Samia suluhu Hassan amesema anajivunia kuwa na mwanamke kwa sasabu ni mfano bora toka alipoanza uongozi mpaka sasa hivyo ni mfano mzuri wa uongozi si Tanzania tu bali duniani.

Aidha amesema kuwa kipindi cha nafasi kumi 10 Rais Samia amewateua walemavu kutokana na uwezo mkubwa na kwamba viziwi wanatambua kuwa nao wana vigezo na wana elimu nzuri na wana tambua kuwa nini kinatakiwa kifanyike na kusema kuwa wakati mwingine jamii inawaangalia watu wenye ulemavu kama mzigo.

Festo Sikagonamo ni Mkurugenzi wa taasisi ya (ELIMISHA) amesema kuwa katika mkutano huo ulijumuisha wanawake , watu wenye ulemavu pamoja na vijana na kushukuru Internews kupitia mradi wao wa boresha habari baada ya kuona shughughuli mbalimbali zinazofanywa na Elimisha .

Mkurugenzi huyo amesema lengo la kufanya mdahalo huo ni kutokana na mwamko mdogo kwa wenye ulemavu, wanawake pamoja vijana kutokuwa na mwamko kushiriki kwenye nafasi mbalimbali za uongozi.

Jane Dusu (51) ni mlemavu wa miguu amewataka watu wenye ulemavu kuacha woga na kugombea nafasi za uongozi,na kwamba mwaka 2025 ni uchaguzi wajitokeze kwa wingi kugombea nafasi mbali mbali ambazo zitatangazwa ndani ya chama ,hakuna sababu ya kujiweka pembeni kutokana na ulemavu wao.