September 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

‘Tukafanye siasa za kujenga sio matusi’

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Dar es Salaam

VYAMA vya siasa vimetakiwa kuendesha siasa za kujenga majukwaani na sio kutukanana ili Tanzania iendelee kuwa mfano wa kuigwa.

Rais hiyo imetolewa na Rais Samia Suluhu Hassan Ikulu jijini Dar es Salaam jana alipokutana na viongozi wa vyama 19 vyenye usajili wa kudumu na kutangaza kufuta tangazo la zuio la mikutano ya vyama vya siasa.

Alisema ni wajibu wa vyama vya siasa kufuata sheria na kanuni zinavyosema. “Kama Watanzania tunatoa ruhusa za mikutano ya vyama vya siasa tukafanye siasa za kujenga na sio kubomoa.

Tukafanye siasa za kistaarabu. Sisi ndani ya CCM tunaamini kukosoa na kukosolewa,” alisema Rais Samia na kuongeza;

Mnikinikosoa mnaniambia nikajikosoe na mkinikosoa nikajikosoa mimi naendelea kuwepo.

Tusiende kutukanana. Kutukanana sio mila zetu, huo sio utamaduni wa Watanzania. Mnaweza mkamtukana Samia Suluhu anaweza kuwa mstamilivu, tunakwenda nchi iko vizuri, akastahimili, lakini chawa wake hawezi kustahimili, akaenda akavaana na chawa wako ikawa balaa,” amesema.

“Lakini ukisema waliahidi barabara kutoka Kakonko sijui kwenda wapi hajajengwa, namuita Mbarawa (Waziri wa Ujenzi) nenda ukafanye hilo, basi na sisi tukiishaijenga tunajua hautakuwa na lingine la kusema” amesema na kuongeza:

“Tukianza kushambuliana kurusha makashifa nchi itakaliwa? Niwaombe sana, fursa imetolewa tusiitumie vibaya, irekebishe Serikali, ishauri Serikali.”

Amesema pale wanapofanya mazuri wasiache kusema. “Najua mtasema Serikali ina madeni, lakini mueleze imefanya nini. Uongo haujengi, lakini kweli unajenga.