July 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TTCL ipo tayari kufanya ushirikiano na wawekezaji nchini

Na Penina Malundo, Timesmajira

SHIRIKA la Mawasiliano Tanzania (TTCL),imesema kwa sasa ipo tayari kufanya ushirikiano na wawekezaji nchini kwa lengo la kuhakikisha wanapaga huduma nzuri ya Mawasiliano.

Pia imesema imejipanga kufungua milango ya kidigitali kwa wawekezaji ili waweze kufanya biashara kwa usahihi zaidi bila kukumbana na changamoto yoyote.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam wakati wa maonesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam ”Sabasaba” Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TTCL Zuhura Muro alisema shirika lao lina wajibu mkubwa wa kuunganisha Mawasiliano mahali popote ili kurahisisha biashara kufanyika kwa usahihi.

“Shirika tunafungua milango ya kidigitali na nchi zinazotuzunguka hivyo tunao mkakati wa kuunganisha Tanzania dunia kidigitali kutokana na nguvu ya Mawasiliano waliyonayo,”amesema Muro

Amesema kupitia ushirikiano waliokuwa nao utawawezesha wawekezaji kufanya shughuli zao mbalimbali bila kupata changamoto zozote na kurahisisha biashara kufanyika vizuri.

Amesema kwa kuwa TTCL imekuwa ikiendesha mkongo wa Taifa hivyo wamejipanga kuhakikisha wanaendesha biashara kila sehemu .

Aidha amesema wanatarajia kuwa kitovu cha malipo jamii na katika kusapoti utalii wanatarajia kupeleka Mawasiliano katika mlima Kilimanjaro.

Amesema hadi sasa jumla ya watalii 9000 wamejiunga na wifi katika mlima Kilimanjaro hivyo wamejipanga vizuri kufungua milango ya digitali kuendesha biashara.