May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TPC Ltd watoa msaada wa chakula cha mifugo vijijini

Na Martha Fatael, TimesMajira Online, Moshi.

KIWANDA cha Sukari TPC Ltd wilayani Moshi kupitia shirika lake la FTK kimetoa msaada wa chakula Cha mifugo Bello 8000 yenye thamani ya zaidi ya mil 60 kwa ajili ya vijiji nane vinavyozunguka kiwanda hicho.

Msaada huo unafuatia vifo vya mifugo zaidi ya 300 kila siku katika baadhi ya vijiji vya kata ya Arusha chini kikiwamo Kijiji Cha Mawala wilayani humo.

Kaimu afisa Mtendaji utawala wa Kiwanda Cha Sukari TPC Ltd, David Shilatu amesema chakula hicho kitagawanywa kwa Serikali za vijiji ili waweze kuwagawanyia wafugaji kwenye maeneo yao.

Amesema msaada huu umetolewa na TPC kupitia shirika lake la FTK kwa vijiji jirani na Kiwanda kama sehemu ya kuwasaidia kipindi hiki mifugo yao inakufa kwa kukosa malisho.

“Mvua za vuli zimenyesha chini ya kiwango kuliko kipindi chochote kilichowahi kutokea na wafugaji walitushirikisha changamoto ya malisho inayowakabili kwa sasa, mifugo imekufa sana ndio maana tukafanya uamuzi wa kusaidia Ufugaji” anasema.

Kwa upande wake Katibu wa mifugo Kijiji Cha Mawala Salimu amesema wafugaji wamepata hasara hali inayosababisha kuwa na hali mbaya kiuchumi.

Amesema msaada wa majani hayo ni malisho ya mifugo ya zaidi ya 30,000 waliopo kwenye maeneo yao ingawa bado wanauhitaji mkubwa.

Naye Meneja wa mradi wa FTK,Nina Sharif amesema kupitia shirika hilo wamefanikiwa kuisaidia jamii katika Miradi ya Elimu, Afya, Kilimo, Miundombinu na Ufugaji ikiwa ni sehemu ya ujirani mwema.

Awali diwani wa kata ya Arusha chini, Leonard Waziri amekiri mifugo mingi kufa kwa kukosa malisho na tayari kata imemuagiza mtaalum wa mifugo kutoa takwimu ya Mifugo iliyokufa.