May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TPC ilivyoongeza uzalishaji wa sukari,Serikali yaridhishwa na uwekezaji wake

“Sisi wawekezaji tumefurahi na kuridhishwa na ufanisi katika uendeshaji wa kiwanda hiki cha sukari cha TPC Limited, ufanisi huu unatoka na faida iliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2022/23 ambapo kiwanda kimeweza kuzalisha faida baada ya kodi ya shilingi 72.7. bilioni kutoka katika mauzo ya shilingi bilion 235 huku gawio kwa wanahisa ikiwa ni shilingi bilioni 69.9” hayo yamesemwa na Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu baada ya kikao cha wanahisa kilichofanyika jana mkoani Kilimanjaro

Mchechu anasema tangu mwaka 2000 kiwanda hiki kimekuwa kikiongeza uzalishaji mwaka hadi mwaka ambapo kwa sasa uzalishaji wa sukari umeongezeka kutoka Tani 36,000 za mwaka 2000 hadi kufikia Tani 116,700 kwa mwaka huu.

Mchechu anaeleza ongezeko hilo la uzalishaji wa sukari limetokana na ongezeko la mavuno ya miwa ambapo kwa mwaka huu kiwanda kimevuna miwa zaidi ya Tani 1,150,000.

“Katika uzalishaji wa sukari kwa mwaka huu, TPC Limited imezalisha zaidi ya tani 116,700 katika kipindi cha juni 2022 hadi machi 2023, hiki ni kiwango kikubwa sana cha sukari  ambacho hakijawahi kuzalishwa katika miaka yote tangu TPC Limited kuanza uzalishaji wake mwaka 1936”.

Anasema wakati wanafanya ubinafsishaji wa kiwanda hicho, serikali ilikuwa imeweka malengo shamba la TPC baada ya kuwa imeongezewa  eneo la shamba la Kahe,  itaweza kuzalisha tani 750,000 kwa mwaka, lakini kwa sasa wanazalisha Tani 1,150,000 ambayo ni juu ya malengo waliyokuwa wamewekwa na serikali wakati wa ubinafsishaji.

“Eneo lile lile lakini uzalishaji unazidi kuwa mkubwa kutokana na tija katika uzalishaji kwani kwa mwaka huu  TPC tumeweza kutoa tija ya wastani wa tani 148 (tani mia moja na arobaini na nane)  kwa hekta kiwango ambacho ni cha juu barani Afrika, na ni moja kati ya viwango bora vitatu duniani” anasisitiza Mchechu

Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu(katikati) , Afisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Sukari cha TPC, Marius Jacobs, (kulia) pamoja na Afisa Mtendaji Utawala wa TPC, Jaffari Ally
wakifuatilia kwa umakini maswali ya waandishi wa habari (hawapo pichani) katika mkutano na vyombo vya habari jana  baada ya mkutano mkuu wa wanahisa uliofanyika mkoani  Kilimanjaro
.

Akizungumzia sababu ya ufanisi na mafanikio hayo, Mchechu anasema Serikali ya awamu ya sita imeweka nguvu na jitihada kubwa za kuhamasisha kilimo na kuvutia uwekezaji katika kilimo hususani katika sekta ya sukari na hilo limeweza kufungua fursa nyingi kwenye sekta ya sukari nchini.

Anasema mambo ambayo yamefanyika katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita ni pamoja na kuendelea kulinda soko la ndani dhidi ya sukari zinazoingizwa zenye kiwango cha chini na kuja kushindana na sukari inayozalishwa nchini yenye kiwango bora.

Anaeleza kuwa kitendo hicho kimefanya sukari kuendelea kuuzwa katika bei nzuri na hivyo kuhamasisha wazalishaji wa sukari kuendelea kuwekeza zaidi katika soko la sukari.

“Tumeshuhudia serikali imekuwa na mfumo unaoeleweka na endelevu wa uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi na hii ni kutokana na maboresho yaliyofanyika katika sheria ya sukari pamoja na kanuni zake ambapo uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi, umewekewa utaratibu mzuri zaidi”.

Anasema eneo lingine ambalo serikali imefanya ni kuhamasisha na kuhakikishia wawekezaji mazingira mazuri ya uwekezaji hali ambayo imechangia kupanda kwa idadi ya wekezaji kutoka ndani na nje ya nchi wanaowekeza katika sekta ya sukari.

“Vipo viwanda mbavyo vimeanza kufanya kazi lakini pia kuna viwanda vingine vinakuja kuweza kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, hivyo katika mazingira haya tumeona serikali ya awamu ya sita, imesukuma mbele jitihada za kukuza kilimo hususani cha miwa, ili kuongeza uzalishaji wa sukari hapa nchini”

Anasema katika kuunga mkono jitihada hizo za serikali, TPC kwa mwaka huu wanatazamia kuwekeza fedha Dola 45 milioni hadi 50 milioni kwa kujenga kiwanda kipya cha kuchakata Molasses ambayo imekuwa ikibaki baada ya uzalishaji wa sukari

“Bodi yetu leo itaidhinisha matumizi ya fedha zaidi ya Dola 45 milioni ama Dola 50 milioni kwa ajili kuweka kiwanda kingine cha uchakataji Molasses na kuweza kuzalisha bidhaa nyingine ambayo itakuwa ni spirit kwa ajili ya matumizi ya viwanda na watumiaji wengine”.

Anasema kiwanda hicho kitajengwa TPC na ujenzi wake unatarajiwa kuanza mapema 2024, na kwamba hicho ni kiwango kikubwa cha fedha kitakachowekezwa ambapo ni pamoja na kukuza zao la miwa na bidhaa zinazotokana na zao la miwa.

Anaeleza kuwa uwekezaji huo kwa TPC utakuza ajira pamoja na kuongeza mapato ya ndani ya kiwanda na kuwezesha kulipa kodi nyingi zaidi na manufaa mengine yatakayopatikana kutokana na uwekezaji huo.

Anasema kubwa zaidi kutakuwa na ongezeko la uzalishaji wa nishati ya umeme ambapo katika kiwanda hicho wanatarajia kufunga mashine nyingine ya kuzalisha umeme na hivyo kutakuwa na ziada ya megawati Nne hadi saba ambazo zitaingizwa katika gridi ya Taifa.

Akizungumzia mchango wa Kiwanda cha Sukari cha TPC kwa jamii, Jafarry Ally ambae ni Mkuu wa Utawala katika kiwanda hicho anasema TPC imeweza kulipa kodi, ushuru pamoja na gawio kwa serikali zaidi ya Sh 99 bilioni, kiwango ambacho ni kikubwa ukilinganisha na kiwango cha Sh 2 bilioni kilichokuwa kikitolewa wakati kampuni hiyo imebinafsishwa mwaka 2000 na sababu kubwa ya kuongezeka kwa kiwango hicho ni uzalishaji,mauzo mazuri na ulipaji sahihi wa kodi kwa mujibu wa sheria na miongozo ya ulipaji kodi.

“Mwaka 2010 ndipo kiwanda kilianza kulipa gawio serikali na hadi mwaka 2022/2023 tumekuwa tukilipa gawio na kiwango kimekuwa kikiongezeka mwaka hadi mwaka na kuifanya TPC kuongoza kwa miaka mitatu mfululizo kwa kutoa gawio zuri na kubwa serikalini kuliko mashirika mengine yote ambayo serikali ina hisa kidogo”.

Akizungumzia mchango wa kiwanda hicho kwa jamii  Ally anasema kwa kupitia shirika lao lisilo la kiserikali la FTK, wamekuwa wakitumia  Sh1.2 bilioni kwa mwaka kwa ajili ya kuhudumia jamii ya vijiji vinavyowazunguka ambapo fedha hiyo inaelekezwa kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta za elimu, afya, miundombinu na miradi endelevu ya vijiji kama miradi ya umwagiliaji.

“Kwa upande wa utoaji wa huduma katika vijiji vinavyotuzunguka tumeendelea kuboresha huduma na kwa upande wa elimu, hivi karibuni tumejenga shule ya sekondari ya Chekereni/Weruweru (CHEWE) ambayo ni ya serikali, na serikali ilituletea fedha za uviko ikaja kuongezea majengo ambayo imefanya shule hiyo kuwa na vitu vingi vilivyokamilika”

“Ni shule inayoanza lakini ina vitu vyote muhimu ikiwemo madarasa, vyoo, jiko, madawati, maabara zote pamoja na jengo la utawala na shule hii itazinduliwa hivi karibuni baada ya serikali kukamilisha uwekaji wa samani”

“Lakini pia tumeweza kutoa huduma za afya na kujenga mundombinu ya barabara kutokana na uwezo tunaokuwa nao ikiwa ni pamoja na kuchimba visima na kujenga mabwawa ya kuoshea mifugo katika vijiji vinavyotuzunguka”.