May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DICOCO yatoa elimu kuhusu kisukari kisarawe

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

TASISI inayojihusisha na utoaji elimu ya ugonjwa wa kisukari kwa jamii( DICOCO)imetoa elimu kwa wananchi wa Wilaya za Bagamoyo na Kisarawe mkoani Pwani kuhusu ugonjwa wa kisukari sambamba na kujiepusha na dalili za ugonjwa huo.

Mbali ya kutoa elimu kuhusu ugonjwa wa kisukari, taasisi hiyo imetoa huduma ya kupima kisukari, shinikizo la damu, urefu na uzito kwa wananchi hao pamoja na kuwakumbusha umuhimu wa kupima afya zao mara kwa mara.

Akizungumza na waandishi wa habari Mwanzilishi wa Taasisi ya DICOCO ambaye pia anaishi na ugonjwa wa kisukari Lucy Johnbosco akieleza sababu za kutoa elimu ya ugonjwa huo na kutoa huduma ya kupima magonjwa bure amesema mwezi wa 11 kila mwaka ni mwezi wa kutoa elimu.

Pia ni mwezi wa kusambaza uelewa , kueneza na kutoa hamasa kwa jamii ili waweze kujua ugonjwa wa kisukari lakini maadhimisho ya ugonjwa huo hufanyika kila Novemba 14, hivyo kama taasisi ya kutoa elimu ya ugonjwa wa kisukari kwa jamii wametumia nafasi hiyo kutoa elimu hiyo ya ugonjwa wa kisukari.

Pia wametoa huduma kupima kisukari na maradhi yote yanayoambatana na ugonjwa huo huku akieleza kuwa walianzia katika Hospitali ya Wilaya Bagamoyo lengo likiwa kuwafikia wananchi wengi wanaotoka katika hospitali mbalimbali.

“Tumewaelimisha na kuwahudumia mama wajawazito, wenye watoto, watu wenye shida ya akili, Waraibu wa Dawa za kulevya pamoja na makundi mengine ya rika mbalimbali.Tukawaelimisha tukawapima sukari, uzito , urefu, tukaangalia uwiano na uzito na urefu wao…

” Tukawaelimisha namna gani ya kuepuka ugonjwa wa kisukari, tukawaelimisha namna gani wanaweza wakala chakula killichokuwa bora na chakula ambacho kinaafya zaidi pamoja na umuhimu wa makundi yote ya vyakula, “amesema.

Ameongeza kuwa baada ya kutoka Hospitali ya Wilaya Bagamoyo, walienda Hospitali ya Wilaya ya Kisarawe ambako nako walitoa huduma mbalimbali kwa wananchi wa makundi yote.

“Novemba 14 tulienda Hospitali ya Wilaya ya Kisarawe ambako tulikusanya kliniki zote tukawaweka pamoja lakini hata watu wa nje walikuja na wanajamii, wamehamasika.Watu Kisarawe na Bagamoyo wanaomba twende tena, ” amesema.

Aidha amesema pamoja na kuendelea kuihudumia jamii ya Watanzania, taasisi ya DICOCO ingependa kupata ufadhili zaidi na watu kuamini kuwa taasisi hiyo inaweza kuleta matokeo chanya.”Kwahiyo wasiogope kutupa msaada na kutuwezesha ili tuendelee kufanya hii kazi ya kijamii.

“Lakini kauli mbiu ya mwaka huu ya mwezi huu wa kisukari inasema Jua hatari za ugonjwa wa kisukari ili uweze kujua namna gani ya kuziepuka.Wakati tunatoa elimu kwa wananchi tulikuwa tunakazia katika dalili za ugonjwa wa kisukari pamoja na madhara yanayotokana na ugonjwa wa kisukari ili watu wajue namna gani wanaweza kuziepuka, ” amesema.