April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TFRA yawatahadharisha wakulima kutumia mbolea kiholela

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

MAMLAKA ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA),Kanda ya Kati imewataka wakulima kuacha kutumia Mbolea kiholela na badala yake waende kujifunza na kupata ushauri wa aina ya mbolea na matumizi yake kwa usalama wa mazao yao.

Hayo yamesema jijini hapa leo na Kaimu Meneja wa TFRA Kanda ya Kati Joshua Ng’ondya wakati akizungumza na Timesmajira kwenye banda la Mamlaka hiyo katika maonesho ya 28,Kanda ya kati yanayofanyika katika viwanja vya nanenane eneo la Nzuguni.

Ng’ondya ameeleza kuwa mbolea ninkirutubisho au mchanganyiko wa virutubisho ambavyo mmea huhitaji ili iweze kuishi,kukua na kuzalisha hivyo ni vyema mkulima akatambua aina ya mbolea anayotumia na wakati gani anapaswa atumie.

“Nawakaribisha wananchi wote wa kanda ya kati na sehemu zingine zote kufika katika banda letu ili waweze kujifunza teknolojia mbalimbali kuhusu TFRA kama kanda ya kati tumekuja na mbolea za aina tofauti tofauti ili wakulima waweze kuziona na kujifunza kwasababu kuna mbolea za kupandia,kukuzia na mbolea kwajili ya Mbogamboga,”amesema.

Amesema kuwa ili wakulima waweze kuzalisha kwa tija wanatakiwa wajue namna ya kutumia mbolea na kwa wakati upi.

“Tunasema kilimo ni biashara,sasa kama kilimo ni biashara namna gani basi ndiyo wananchi wanatakiwa waje katika banda letu ili wajifunze matumizi sahihi ya mbolea hapa ili wazalishe kwa tija na kufanya mazao yao kuwa mazao ya biashara,”amesema.

Pamoja na hayo Ng’ondya amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kwakutoa bilioni 150 ruzuku ya mbolea kitendo ambacho kitaenda kumnufaisha mkulima kutokana na mbolea kuwa bei kubwa na kupelekea wakulima kushindwa kumudu gharama hizo.

Kutokana hilo Ng’ondya amewahimiza wakulima kwenda katika ofisi za Watendaji wa mtaa au Kijiji ili waweze kusajiliwa kwajili ya kupata mbolea ya ruzuku.

“Mkulima akienda kusajiliwa atapewa namba maalumu ya usajili ambayo itamwezesha kwenda kwa wakala waliosajiliwa kuuza mbolea za ruzuku na kunufaika moja kwa moja na ruzuku iliyotolewa na Serikali,”amesema Ng’ondya.

Aidha ametaja faida za kutumia mbolea zinadhibitiwa TFRA kuwa ni kuhakikishiwa ubora wa mbolea hizo na kumfanya mkulima kupata tija iliyokusudiwa kwasababu moja ya majukumu yao ya msingi ni kuzisajili hizo mbolea zote na mkulima anapata mbolea bora.

Kwa upande wake Afisa Udhibiti Ubora wa TFRA kanda ya kati Salvatory Kalokora amesema mtu yoyote haruhusiwi kufanya biashara ya mbolea bila kuwa na leseni.

Kalokora amesema ili kumruhusu mfanyabiashara kuuza mbolea TFRA imeanzisha mfumo wa kidigitali wa usajili wa wafanyabiashara wa mbolea(Digital Platform).

Amesema mfumo huo utamuwezesha mfanyabiashara yeyote kuingia katika mfumo akiwa nyumbani au mahali popote akaingia na kuweka taarifa zake akapatiwa leseni.

“Sisi kama wataalam wa TFRA tunapitia kisha tunamtengenezea leseni tunamtumia anaipata vilevile kwenye mfumo na akiingia anachukua leseni yake anaweka dukani,hivyo mamlaka inahamasisha wafanya biashara wote kuhudhuria mafunzo na kupata cheti cha mafunzo ya mbolea ili waweze kuuza mbole kwa utaalam,”amesema.