May 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TBL kuendelea kuwa wabunifu katika soko la vinywaji

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Kampuni ya Tanzania Breweries Public Limited (TBL) inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuhakikisha wanaendelea kuwa imara katika soko la vinywaji kwa kufanya ubunifu kwenye utengenezaji wa vinywaji vyao pendwa hapa nchini.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi wa kampuni hiyo Leonard Mususa wakati akizungumza kwenye Mkutano Mkuu wa 50 wa Wanahisa wa TBL leo Jijini Dar es Salaam.

“Tunaendelea kuwa wabunifu kwa kuleta vinywaji kwa ajili ya wanywaji wetu wote, kuna vijana na wazee na wote wanapenda vinywaji tofati, hivyo kwa ujumla tunaangalia jamii inapenda nini kwa kufanya tafiti kwenye soko.”

Pamoja na hayo amezungumzia mkakati wa TBL wa kuanzisha kiwanda cha kuchakata Shairi ambacho kinajengwa Moshi mkoani Kilimanjaro na matarajio yao Machi mwakani kitaanza uchakataji wa shairi.

“Hivi sasa tunatumia shairi tani 5000 lakini kiwanda kikianza uzalishaji tutafika tani 12000 na katika kipindi cha miaka mitano ijayo tutakuwa tumefika uzalishaji wa shari tani 3200 na zote hizo itabidi zipatikane.”

“Hivyo tutaongeza uzalishaji kwa wakulima, kwa sasa shairi inapatikana Arusha ,Manyara na West Kilimanjaro lakini tunatarajia pia ianze kulimwa katika mikoa ya nyanda za juu Kusini ambako nako hali yake inaruhusu.”

Mbali na hayo Mususa amesema Kampuni hiyo imetoa gawio la jumla ya Sh.bilioni 85 zimetolewa kwa wanahisa wake ambapo thamani ya hisa moja ni Sh.290.

Amesema kutokana na faida waliyoipata gawio kwa wanahisa limeongezeka kutoka Sh.255 kwa hisa moja hadi Sh.290 kwa hisa moja.

“Tunalipa zaidi kutokana na faida tunayoipata , kampuni yetu tumetoka kupata faida ya Sh.bilioni 134.7 mpaka Sh.bilioni 153.4 na ndio maana tumeweza kulipa kiasi hicho cha Sh.290 kwa wanahisa wetu.Mwaka 2022 kidunia ulikuwa na changamoto nyingi tumeona vita kati ya Urusi na Ukraine.

“Misukosuko na kutoelewa kwa mataifa mbalimbali , mfumo wa bei duniani kote umekuwa mkubwa, hapa kwetu nafuu kidogo , riba ziko juu, hizo changamoto zote tunaziona hata sisi.

“Ukiangalia katika utendaji gharama zetu utakuta ziko juu kutokana na usafirishaji wa bia lakini ukiangalia ripoti yetu ya mwaka ya utendaji, ukiangalia mauzo yetu mauzo yameongezeka kwa asilimia 12,”amesema.

Ameongeza pamoja na changamoto hizo hali ya utendaji ya TBL iko vizuri, mauzo yameongezeka , faida imeongezeka zaidi na hiyo inatokana na udhibiti wa gharama kwenye utendaji lakini pia ufanyaji kazi kwa tija zaidi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TBL Jose Moran amewahakikishia wanahisa wote kuwa kampuni hiyo inaendelea kutengeneza vinywaji vinavyopendwa nakutoa vinywaji kulingana na makundi mbalimbali.