October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tanzania yaadhimisha Siku ya Takwimu Duniani

Na Joyce Kasiki,TimesMajira Online. Dodoma

TANZANIA imeungana na nchi nyingine duniani kuadhimisha Siku ya Takwimu, ambayo hufanyika kila baada ya miaka mitano huku ikielezwa kuwa kwa hapa nchini, serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuendeleza na kuimarisha mifumo ya Takwimu.

Hayo yamesemwa jijini hapa na Mtakwimu Mkuu, DKt. Albina Chuwa wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo amesema, ofisi yake imeendelea kuboresha uwezo na kuimarisha takwimu nchini katika Wizara, Idara na taasisi za serikali kupitia mpango wa kwanza wa kuboresha na kuimarisha takwimu nchini.

Vile vile amesema Tanzania, imepunguza gharama kwa kufanya tafiti kwa kutumia teknolojia za kisasa na kuondokana na mfumo wa kutumia makaratasi.

Katika hatua nyingine, amesema serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya uzalishaji wa takwimu na kuendana na wakati.

Dkt. Chuwa ametumia fursa hiyo kuwataka wadau wote kutumia takwimu katika mipango yao ya maendeleo na taifa kwa ujumla.

“Baada ya takwimu kuzalishwa, zinakuwa ni mali ya umma lakini changamoto kubwa iliyopo wadau hawatumii takwimu, sisi wote ni wadau wa takwimu na si serikali peke yake,” amesema.

Juni 3, 2015 Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UN) lilipitisha Azimio namba 69/289, ambalo liliamua siku ya Oktoba 20 ya kila mwaka kuwa maadhimisho ya Siku ya Takwimu Duniani.