May 12, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tanzania, China kufungua fursa za biashara, uwekezaji

Na Iddy Lugendo, Timesmajira Online DSM

SERIKALI ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha fursa za uwekezaji na Diplomasia ya kiuchumi jambo ambalo limepelekea kuwavutia kwa kiwango kikubwa wafanyabiasha na wawekezaji kuwekeza nchini.

Akizungumza wakati wa kongamano la wafanyabiasha kutoka China Julai 03, 2023 jijini Dar es Salaam Naibu Waziri Wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Mheshimiwa Exaud Kigahe amesema lengo la mjadala huu ni kufungua fursa mbalimbali zilizopo baina ya Tanzania na China.

Naibu Waziri Kigahe amesema kwa ushirikiano huu wa china tunajenga kituo cha biashara cha Afrika mashariki pale Ubungo, litakuwa ni soko kubwa au lango kwa biashara nyingi au bidhaa jambo ambalo litapelekea kwa wafanyabiasha mbalimbali kutokwenda tena China kwaajili ya kuchukua bidhaa hizo.

Aidha, Kigahe amesema uwekezaji huo utachangia kupunguza gharama kwa wafanyabiasha mbalimbali nchini na kuokoa muda, hivyo amewataka Watanzania kuungana na wachina kwa sababu soko hilo litahudumia ukanda mzima wa Afrika mashariki na kati kwa kushirikiana na Watanzania katika uwekezaji wa miradi mbalimbali ambayo itakuwa na tija kwa uchumi Taifa letu.

Naye Rais wa Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Edmund Mkwawa amesema kuwa uhusiano huu wa kibiashara utazinufaisha nchini zote kwa Watanzania kwenda china kuwekeza na wachina kuja hapa kuwekeza kutokana na mazingira wezeshi ya uwekezaji ambayo Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake meneja wa EACLC inayodhamini maonesho ya sabasaba, Wang Xiangyu amesema kuwa kampuni zaidi ya 50 kutoka china kuhudhuria maonesho ya sabasaba wamekuja kuonesha na kutambulisha kampuni zao jambo ambalo litaendeleza ushirikiano mzuri kwa nchi zote mbili na hivi sasa maonesho ya sabasaba ni maarufu sana kule china hivyo tunaamini watu wengi watafika kutembelea banda la china.