May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TANTRADE yashiriki Kongamano Oman

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) kwa kushirikiana na Ubalozi wa Tanzania nchini Oman wamefanikiwa kuratibu na kushiriki Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Oman lililofanyika tarehe 13 Juni, 2022 katika jiji la Muscat.

Kongamano ni sehemu ya Ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan ambapo zaidi ya watu 300 kutoka Sekta Binafsi na Umma wameshiriki.

Aidha kwenye kongamano hilo, jumla ya mikataba (MoUs) 6 ilisainiwa ambapo 4 ni ya Sekta ya Umma na miwili kwa Sekta Binafsi.

Katika Kongamano hilo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amewahakikishia wa wafanyabiashara wa Oman mazingira mazuri ya biashara ikiwa ni pamoja na sera thabiti za fedha.

Rais Samia Suluhu Hassan amesema kuwa tangu achukue madaraka, Sera ya Serikali yake ni kuacha Serikali iongoze na Sekta Binafsi ifanye Biashara.

Rais Samia Suluhu Hassan aliahidi kuendelea kutatua changamoto zinazowakabili wafanyabiashara akishirikiana na Serikali ya Oman.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade Bi.Latifa Mohamed Khamis amesema kuwa , Tantrade itaendelea itaendelea kuratibu makongamano ya Biashara na kuhakikisha wafanyabiashara wa Tanzania wanaunganishwa na wafanyabiashara wa Oman ili kupata soko la bidhaa na kuendeleza Biashara hizo.

Sambamba na Kongamano hilo pia lilifanyika Kongamano la watanzania waishio Oman (Diaspora) ambapo walipata fursa ya kuelezwa fursa mbalimbali zilizopo Tanzania na pia kuwasilisha changamoto zinazowakabili kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye aliahidi kufanyia kazi changamoto hizo.