May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TANTRADE yashiriki kongamano la biashara kati ya Tanzania na Indonesia

Na Mwandishi wetu, Timesmajira Online

MAMLAKA ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) imeratibu na kushiriki kwenye Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Indonesia lililofanyika tarehe 25 Januari, 2024 katika jiji la Jakarta.

Kongamano hilo ni sehemu ya Ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ilioanza tarehe 24 Januari, 2024 yenye lengo la kuendeleza na kukuza mahusiano ya kiuchumi kati ya nchi hizi na hasa kuhamasisha biashara na Uwekezaji kwa pande zote mbili.

Taasisi mbalimbali za Sekta Binafsi na Umma pamoja na wafanyabiashara kutoka Tanzania wamekutana na wenzao wa Indonesia kubadilishana fursa baina yao.

Katika Kongamano hilo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan amewahakikishia wafanyabiashara wa Indonesia na Tanzania mazingira mazuri yatakayoendelea kukuza biashara baina ya nchi hizi mbili ikiwa ni pamoja na sera thabiti za kisiasa na uchumi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade, Latifa Mohamed Khamis pamoja na Bw. Soegeng Hernowo, Mkurugenzi Mkuu wa PT PPI walisaini na kubadilishana Hati ya makubaliano ya ushirikiano katika ukuzaji biashara kwa nchi zote mbili.

Mkurugenzi wa TanTrade pia alitumia fursa hiyo kuainisha fursa za biashara zilizopo Tanzania na kueleza kuwa TanTrade itaendelea kuibua fursa kwa wadau wa biashara nchini na kuratibu mikutano ya Biashara na kuhakikisha wafanyabiashara wa Tanzania wanaunganishwa na wafanyabiashara wa Indonesia ili kupata soko la bidhaa zinazozalishwa nchini