April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Taasisi zaungana kuwapatia taarifa sahihi za Afya ya uzazi wanafunzi wa Shule za msingi

Na Penina Malundo

TAASISI ya Msichana Initiative,Binti Salha na Mtandao wa Kimataifa wa Wanawake wa Haki ya Afya ya Uzazi (WGNRR Africa),zimeungana katika kutoa elimu ya afya ya uzazi na jinsia kwa wanafunzi wa shule za msingi,kwa lengo la kuwapatia taarifa sahihi za elimu hiyo ili waweze kujilinda na kujitambua.

Akizungumza hayo jana jijini Dar es Salaam ,Mkurugenzi wa Taasisi ya Binti Salha,Salha Azizi,wakati wa warsha ya utoaji wa elimu hiyo kwa wanafunzi na walimu wao, alisema kundi la watoto wa shule ya msingi ni miongoni mwa kundi hatari ambalo linakumbwa na vitendo vya kikatili vingi.

Amesema elimu wanayowapatia wanafunzi hao pamoja na walimu wao itaweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa kujilinda dhidi ya ukatili kama masuala ya ubakaji,ulawiti na kupotezewa ndoto zao katika kusumbuliwa na wanaume wa mitaani.

”Tumeamua kutoa elimu hii ili kutoa elimu sahihi kwa watoto ili kujua namna ya kujilinda wakiwa bado wadogo kwani samaki mkunje angali mdogo wakishakuwa wakubwa wanakuwa wanaelewa kila kitu na kujiepusha na changamoto mbalimbali zinazohusu afya ya uzazi na kuathiri ndoto zao,”amesema na kuongeza

”Tumewapa taarifa za namna ambavyo wanaweza kujilinda wao wenyewe dhidi ya ukatili kama masuala ya ubakaji,ulawiti na kupotezewa ndoto zao na wanaume ambao wanakuwa wanawalaghai kwa zawaidi ndogo ndogo,”amesema.

Aidha amesema mbali na elimu hiyo pia walizungumza na walimu wa wanafunz hao kuhusu umuhimu wa kuwalinda na kuendelea kuwasaidia watoto hao kufikia ndoto zao.

”Tunajua walimu wanamuda mwingi wa kukaa na watoto hawa,hivyo ni vema na wao ni sehemu kubwa ya kuisadia watoto kulelewa na kukuwa katika mazingira mazuri,”amesema na kuongeza

”Tumewasisitiza watoto kuwa wanapofanyiwa vitendo kama hivyo wasiwe waoga kuripoti matukio hayo kwasababu wanaporipoti inawasaidia wao wenyewe kuweza kuwa na ulinzi, kuwalinda watoto wenzao na hao wanaofanya hivyo vitendo kuchukuliwa hatua,”amesema.

Kwa upande wake Afisa Vijana kwenye Program ya Afya ya Uzazi kutoka WGNRR Africa,Walta Carlos amesema kundi la mabinti wamekuwa wakipitia changamoto za ukatili wa kijinsia hasa ukatili wa kingono unaopelekea mimba ya utotoni hata ndoa za utotoni.

Amesema ukatili wa kingono ni moja ya sababu inayomuathiri mtoto katika afya ya uzazi kwa kupata mimba za utotoni na kukatisha ndoto zao za kuendelea na masomo.

Naye Afisa Utawa kutoka Taasisi ya Msichana Initiative,Agness Tillya Agness amesema warsha hiyo imeunganisha watoto hao kutoka shule mbalimbali mkoani Dar es Salaam ambazo wamekuwa wakiendesha klabu mbalimbali za Msichana Amani ni jukwaa la watoto kuanzia miaka 10 ambapo watoto uelezea changamoto zao na kuzitatua wenyewe kupitia mziki na kipima hisia.

Amesema wazazi wengi wamekuwa waoga kuongea na watoto wao hivyo kupitia klabu hizo zitasaidia kwa kiasi kikubwa kupata taarifa sahihi pindi wanavyozidi kukua.

Aidha Mwalimu wa Shule ya Msingi Boma,Nessa Mbwambo amesema kupitia klabu zao wamekuwa wanaongea na wanafunzi hao kwa kuwaelimisha kwa kufatana na mitaala iliyopo shuleni.

”Katika mitaala ya shule,darasa la sita kuna topic inayozungumzia afya ya uzazi hivyo kupitia mitaala hyo tunawafundisha kupitia mitaala na kusema kwa uwazi,”amesema.

Naye Mwanafunzi Mwanafunzi wa Darasa la Saba kutoka Shule ya Mji Mwema, Brigita John(sio jinalake halisi) ,amesema changamoto wanayokutana nayo kubwa ni vijana hasa wa bodaboda kuwasumbua na kutoangalia umri waliokuwa nao.

”Tunashukuru taasisi hizi kuanzisha klabu shuleni ambazo tumekuwa tunaripoti matukio tunayokutana nayo huko mtaani kama vijana kutuitaita wachumba na wengine kutulazimisha kushika miili yetu,”amesema.