April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Taasisi ya Green Kids and Youth Foundation, Victorious waadhimisha siku ya mazingira

Na Heri Shaaban, TimesMajira Online, Ilala

Taasisi zinazoshughulika na maswala ya kijamii ya Green Kids & Youth Foundation na Victorious Health Foundation zilizopo Wilaya ya Ilala Kata ya Kitunda zimeadhimisha siku ya Mazingira Duniani kwa kupanda miti ya vivuli katika shule nne za serikali na Zahanati zote zilizopo katika Kata ya Kitunda tarafa ya Ukonga.

Maadhimisho hayo ya Mazingira ambayo yaliongozwa na Taasisi hizo yalifanyika Kitunda wilayani Ilala , ambapo taasisi hizo zilishiriki na klabu za Mazingira za shule hizo.

Akizungumza katika maadhimisho hayo Mwenyekiti wa Green Kids &Youth Foundation Vaileth Mwazembe alisema taasisi hiyo inashughulika na masuala ya kupinga ukatili kwa vijana watoto na wanawake wameadhimisha siku ya Mazingira Kitunda kwa kushirikiana wanafunzi na wanachama wa taasisi hiyo.

Vaileth alisema kila mwaka wanashiriki siku ya Mazingira Duniani kwa kushirikisha jamii ambapo wanapanda Miti katika taasisi za Serikali na kwenye Miradi ya Serikali katika kuunga mkono Juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan katika suala la utunzaji Mazingira.

Alimpongeza Balozi wa Mazingira Wilaya ya Ilala Heri Shaaban kuendelea kampeni ya Mazingira katika Wilaya Ilala na kampeni yake endelevu ya kupanda MITI.

Alitumia nafasi hiyo kuipongeza Halmashauri ya Jiji kwa kuwapatia miti kwa ajiri ya maadhimisho ya Mazingira Duniani Kata ya Kitunda Wilaya ya Ilala.

Katibu wa Taasisi ya Victorious Health Foundation inayoshughulikia masuala ya Afya kwa vijana Edwin Rumboyo alisema Miti chanzo cha chakula bora pamoja na kivuli. hivyo huwezi kutenga Mazingira na Uhai wa mwanadamu.

Edwin alisema mkakati wa Taasisi ni kuwa na mradi wa Mazingira utakaogusa shule zote za Wilaya ya Ilala msisitizo ni kupanda miti ya Matunda ili kuboresha Afya ya watoto wetu wawapo mashuleni hivyo ameomba wadau wajitokeze kuunga mkono mradi huo.

Akasisitiza kuwa kwa Jamii swala la Mazingira linapaswa kuwa jukumu letu sote sio la mtu mmoja.

Kwa upande Katibu wa Siasa na Uenezi CCM Kata ya Kitunda Bushir Halfan alipongeza taasisi hiyo ya kijamii Kitunda kwa kuwa karibu na Jamii na Chama cha Mapinduzi CCM itakuwa nao pamoja katika kuwashirikisha katika shughuli mbali mbali ikiwemo kuwawezesha ili kufanikisha kampeni za kupinga vitendo vya ukatili katika maeneo ya Ukonga.
Mwisho.