April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Spika: Taarifa tukio la Mbowe zisichelewe

Na Joyce Kasiki, TimesMajira Online, Dodoma

SPIKA wa Bunge, Job Ndugai, amevitaka vyombo vya usalama vitoke mapema na viseme bila kuchelewa kuhusiana na tukio la kushambuliwa kwa Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni (KUB), Freeman Mbowe.

Spika ametoa agizo hilo Bungeni jioni jijini Dodoma wakati akiwaeleza wabunge kuhusiana na tukio la kushambuliwa kwa Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa. Tukio hilo lilitokea saa 6 usiku nyumbani kwake Area D, jijini humo.

“Tukio lenye lina hadithi nyingi inamiwia vigumu kulisemea, lakini niseme tu msilichukulie kama hivyo wanavyosikia…watakaolisemea ni vyombo vya usalama, hivyo naviomba vitoke mapema viseme bila kuchelewa, kwani wanavyozidi kuchelewa hadithi zinazidi kuwa nyingi,” amesema Spika Ndugai na kuongeza;

“Kesho saa kama hizi (leo jioni) tutakuwa na jambo la kusema na niwahakikishie wabunge kwamba Dodoma ni salama kabisa kabisa na tumekaa hapa tangu mwezi wanne na sasa mwezi wa sita hakuna aliyepoteza kilo, jicho wala mkono.”

Spika Ndugai amesema Mbowe amevunjika mfupa wa nyuma wa mguu na kwamba madaktari wamemwambia watampatia ushauri wao baadaye kidogo, lakini wamesema mtaalam wao anaweza kufanyia upasuaji.

Hata hivyo Spika Ndugai amesema wanasubiri kwanza kusikia jinsi madaktari watakavyowashauri.