September 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Shirika la My Legacy wahamasisha kufanya usafi soko la Kawe

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Shirika lisilo la Kiserikali la My Legacy limeshiriki zoezi la kufanya usafi katika soko la Kawe kwa lengo la kuhamasisha wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla kujijengea tabia ya kufanya usafi wa mazingira kwa vitendo bila kusubiri kusukumwa na serikali .

Shirika hilo ambalo dhumuni na lengo lake kubwa ni kujaribu kupunguza umaskini uliokithiri kwenye jamii kupitia kuwezesha makundi mbalimbali kama vile wanawake na Vijana, tayari limeshatekeleza miradi mbalimbali kwa mafanikio makubwa ikiwemo Mradi maarufu wa WASH.

Akizungumza na waandishi wa habari jana baada ya zoezi hilo la usafi katika maeneo mbalimbali ya soko la Kawe Afisa Miradi kutoka shirika hilo Bw. Julius Prinsipatus alisema kuwa shirika la My Legacy linaamini kwamba suala la usafi na utunzaji mazingira ni la wanajamii kwa maana athari zozote zinazotokana na uchafuzi wa mazingira linaifikia jamii moja kwa moja kwahiyo wananchi inabidi wawe mstari wa mbele kusafisha na kutunza mazingira bila kusubiri kusukumwa na serikali.

” Tupo hapa tunahamasisha wanajamii na Uongozi wa sehemu hii kujitolea kufanya usafi na kutunza mazingira ili kuweza kupunguza matatizo mbalimbali yanayotokana na uchafu, tumeshafanya hivi katika maeneo mbalimbali ikiwemo soko la Kunduchi ambapo tulipanda na kuhamasisha upandaji wa miti, Ombi langu kwa serikali ni kwamba tunaiomba iweze kutuunga mkono wadau kama sisi ambao tunajitolea kuhamasisha wanajamii, lakini waweze kuangaliaa sehemu mbalimbali zenye changamoto za uchafuzi wa mazingira na kuzitatua”. Alisema Julius

Aidha aliihamasisha jamii waendelee kujitolea kwani wamaoathirika zaidi ni wanajamii wenyewe.

“Kama kukitokea mlipuko wa magonjwa wanaoathirika ni Wana jamii wa soko hili kwahiyo tunahamasisha wanajamii waendelee kujitolea kwenye maeneo yao”

Kwa upande wake Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa Mzimuni Raiya Nassoro, aliiomba Manispaa kuendelea kuwaboreshea soko lao liendelee kuwa zaidi ya lilivyo sasa kwani soko hilo linategemewa na Kata takribani 4 kwaajili ya kupata mahitaji yao.

Pia aliwaomba wananchi wa Kawe kutoa ushirikiano katika zoezi la usafi ili kuepusha magonjwa ya mlipuko.

Mwenyekiti wa soko la Kawe, Yusuph Abdallah, aliwashukuru My Legacy kwa kuwapa ushirikiano mkubwa hasa kwenye Idara ya Afya tangu kipindi cha ugonjwa wa UVIKO-19 kwa kuwapatia vifaa vya usafi lakini pia sabuni n.k

“Leo hii wanapokuja kutuongezea msukumo wa kuja kushiriki kwenye suala la usafi kwetu limetuamshansha sana, na hii itatusaidia na sisi kuendeleza msukumo huu kufanya usafi huu wa Kila jumamosi kama Serikali yetu inavyotutaka”

Mfanyabiashara Omary Mohammed alilipongeza Shirika la My Legacy kwa kuhamasisha suala la usafi na Utunzaji wa Mazingira katika maeneo mbalimbali Nchini, lakini pia uanzishaji wa Miradi mbalimbali yenye lengo la kuleta mabadiliko chanya katika jamii ya Tanzania.

“Uhamasishaji huu uendelee siyo kwa kawe tu, bali na maeneo mengine mbalimbali” Alisema

Wafanyakazi wa shirika liliso la kiserikali, My Legacy wakiwa pamoja na wananchi wa Kawe, wakifanya usafi katika soko la Kawe Jana ikiwa ni muendelezo wa Kuhamasisha utunzaji mazingira katika maeneo mbalimbali nchini ili kuweza kuepukana na magonjwa ya mlipuko.