*Mradi utakaogharimu zaidi ya tirioni 1
*Ni mgodi wa dhahabu uliopo Sengerema mkoani Mwanza
*Mavunde aeleza kuwa utachochea ukuaji wa uchumi wa nchi
Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza
Serikali ya Tanzania na kampuni ya uchimbaji madini NYANZAGA (NYANZAGA Mining Limited) imesaini mkataba wa makubaliano ya nyongeza kwa ajili ya mradi wa uchimbaji mkubwa wa madini ya dhahabu kupitia kampuni ya ubia ya Sotta Mining Corporation Limited,ambao unaelezwa kuwa kichocheo cha uchumi wa taifa na ustawi wa wananchi.
Utekelezaji wa mradi wa uchimbaji wa dhahabu katika mgodi wa Nyanzaga,uliopo Kata ya Igalula wilayani Sengerema mkoani Mwanza. unatekelezwa kwa ubia kati ya Serikali ya Tanzania na kampuni ya Perseus Mining Limited kupitia kampuni ya NYANZAGA Mining Company Ltd,unaotarajia kuwa kichocheo cha ukuaji wa uchumi wa taifa na ustawi wa wananchi katika kipindi chote cha utekelezaji wake.

Akizungumza Agosti 20,2025,wilayani Sengerema katika hafla ya utiaji saini ,Waziri wa Madini Anthony Mavunde,amesema kutokana na Wizara kuanzisha timu ya majadiliano, katika mkataba huo umiliki wa hisa za Serikali zimepanda kutoka asilimia 16 hadi asilimia 20 huku mbia huyo akiwa na asilimia 80.
Mavunde amesema,uwekezaji huo ni wa zaidi ya tirioni moja na taarifa ya awali ya utafiti unaonesha ya kwamba maisha ya mgodi huo utakuwa ni miaka 12 mpaka 15, ingawa utafiti bado unaendelea huku akisisitiza kuwa wananchi watapata mafanikio na kunufaika kupitia mgodi huo kwa muda wote huo.
“Mradi kama huu ni watu wamekuja kuomba leseni ya utafiti wizarani,wametumia gharama zao,wameleta mtaji wao.Serikali ina kwenda kupata asilimia 20 bila kuchangia senti moja,pia tuna kodi,tozo na ushuru mbalimbali,tunakwenda kunufaika na uwekezaji huu ikiwemo wananchi wa eneo hili na taifa kwa ujumla kwa kutoa fursa za ajira,kukuza pato la Halmashauri ya Sengerema,Mkoa wa Mwanza pamoja na taifa kwa ujumla,”amesema Mavunde.
Pia amesema Serikali imeweka mkazo kuhakikisha wananchi wanashiriki kikamilifu kupitia utoaji wa huduma na bidhaa mbalimbali zinazohitajika kwenye mradi huku kampuni hiyo italazimika kushirikiana na jamii kuboresha huduma za kijamii kama shule, afya, maji na miundombinu pamoja na kusaidia miradi ya maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi.
Sanjari na hayo Mavunde,amesema anatambua kazi zinaendelea ikiwemo ujenzi wa nyumba 262 za wale walioguswa na mradi na tayari nyumba 129 zimekamilika huku idadi kubwa ya wananchi wameisha hamia kwenye nyumba hizo.
“Naitaka kampuni ya Sotta Mining Corporation Limited kuhakikisha kuwa kama mlivyosema Oktoba 31,2025, zoezi ya ujenzi wa nyumba liwe limekamilika na wananchi wote waliopisha mradi waweze kukabidhiwa nyumba zao ili waendelee na maisha yao,”.
Aidha Mavunde ameeleza kuwa kampuni ya Sotta Mining imerudisha leseni yake Serikalini, na Wizara itahakikisha leseni hizo zinagawiwa kwa wananchi wa Wilaya ya Sengerema, huku akihimiza kampuni kuendelea kutoa msaada wa kiufundi kwa wachimbaji wadogo.Pia ameliagiza Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kupeleka mtambo maalum wa kuchoronga (drilling rig) ili kusaidia wachimbaji wadogo kuongeza tija.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Perseus Lee-Anne de Bruin ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kufanikisha mazungumzo hayo na hatimaye kusainiwa mkataba huo wa nyongeza kati ya Serikali na kampuni yao ambapo utaruhusu shughuli za uzalishaji kuanza pindi shughuli za ujenzi zitakapokamilika mwanzoni mwa mwaka 2027.
“Mradi huu utaleta manufaa kwa taifa hili mara baada ya kuanza uzalishaji, na tunatarajia dhahabu ya kwanza kuzalishwa robo ya kwanza ya mwaka 2027,Tunamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza uhusiano mzuri wa kidiplomasia uliosaidia kurahisisha mchakato wa uwekezaji huu mkubwa,” amesema Lee-Anne.
Kwa upande wake Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu,amesema kupitia mgodi huo taifa litapata maendeleo endelevu na faida zaidi kwani ni moja ya miradi mikubwa zaidi ya madini Tanzania,ambao unatarajia kuiingizia Serikali kiasi cha bilioni 400 lakini pia mapato kupitia kodi, gawio na vitu vingine pamoja na kutoa fursa ya ajira kwa wananchi.
“Mradi huu utaimarisha uchumi wetu, katika kipindi cha mnyukano wa uchumi duniani, kilichotusaidia ni madini, ni bidhaa inayotuletea fedha nyingi za kigeni na kusaidia kuimarisha uchumi wetu,”amesisitiza Mchechu.
Naye, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda ameeleza kuwa kiasi cha cha dola za Marekani milioni 500,ambazo zitakazotumika kujenga mradi huo, zitasaidia kubadilisha Mkoa mapato kuongezeka.



More Stories
Clara:Miaka 50 ya Sabasaba fursa mpya za Biashara na Uwekezaji
Usajili wa Laini za Simu: Jilinde Dhidi ya Kutumiwa Vibaya kwa Utambulisho Wako
TTCL yaadhimisha siku ya Wanawake kwa kutoa msaada JKCI