May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu

Serikali yawoamba wadau wa maendeleo kuwaunga mkono

Na Hadija Bagasha, TimesMajira Online, Tanga

SERIKALI imewaomba wadau wa maendeleo nchini kuendelea kuwaunga mkono katika utatuzi wa changamoto za kimaendeleo katika maeneo mbalimbali ikiwemo elimu na afya.

Ombi hilo limetolewa na Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akizindua vyumba vitatu vya madarasa vilivyojengwa kwa ufadhili wa kampuni ya Neelkanth Chemicals Ltd Cha Jijini Tanga.

Waziri Ummy amesema kuwa Serikali pekee yake haiwezi kumaliza changamoto zote zilizopo katika maeneo mbalimbali nchini hivyo wadau wa maendeleo wanategemewa kwa ajili ya kusaidia katika utekelezaji wake.

“Kubwa naloweza kusema niwashukuru Neelkanth kwa kusaidia ujenzi wa madarasa matatu katika shule hii ya Mnyanjani ambapo kwa msaada huu Sasa changamoto ya uhaba wa madarasa imeweza kumalizika”amesema Waziri Ummi.

Waziri Ummy aliwataka wazazi na walezi kuhakikisha wanafuatilia kwa ukaribu masomo ya watoto wao iliwaweze kuwasaidia kupata matokeo mazuri .

“Niwaase wanafunzi kuweka jitihada binafsi katika swala zima la elimu na kuachana na Mambo ya anasa kwani yataweza kuwakatisha ndoto zenu za kufikia elimu Bora”amesema Waziri Ummy.

Awali akisoma taarifa ya mradi huo Mkuu wa shule ya sekondari ya Mnyanjani Saida Mahadhi amesema kuwa kwa kukamilika kwa vyumba hivyo Sasa shule hiyo inajumla ya vyumba 23.

Amesema kuwa kwa Sasa wanakabiliwa na changamoto ya uhaba wa matundu ya vyoo pamoja na ukosefu wa uzio hali inayowawia vigumu kudhibiti nidhamu yawanafunzi.

Naye Mkurugenzi wa kampuni ya Neelkanth Chemicals Ltd Rashid Liemba amesema kuwa msaada huo ni sehemu ya wajibu wao Kama kampuni kurudisha fadhila kwa jamii.

“Msaada ni sehemu ya mipango ya kampuni katika kusaidiana na serikali kutatua changamoto zilizopo kwani tunajua hata sisi ni sehemu ya Jamii hivyo ni wajibu wetu kusaidia”amesema Liemba.