April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yapongezwa uanzishaji mfuko wa fidia kwa wafanyakazi

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

WAFANYAKAZI wameipongeza Serikali kwa uamuzi wake wa kuanzisha Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwani ni msaada mkubwa kwa waajiri hususan linapokuja suala la kusaidia wafanyakazi wanapoumia, kuugua ama kufariki kutokana na kazi.

Wakizungumza kwenye kilele cha Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo Tanzania 2023 maarufu kama Nanenane katika viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya, wamesema wao kama wafanyakazi ndio wanufaika wakuu wa Mfuko huo, baada ya waajiri wao kujisajili WCF.

Dkt. George Mufulu, Mhadhiri Chuo Kikuu Mzumbe, Morogoro, amesema kabla ya kuanzishwa kwa WCF waajiri walikuwa wanaingia gharama kubwa sana kuwahudumia wafanyakazi wao pale wanapopatwa na majanga mbalimbali wawapo kazini.

“Mimi binafsi nimekuwa nikifahamu huduma mbalimbali za WCF kwa kweli Serikali inapaswa kupongezwa kwa uamuzi wake wa kuanzisha chombo hiki, kwa sababu huko nyuma waajiri walikuwa wakiingia gharama kubwa sana kuwahudumia wafanyakazi wao pale wanapokuwa wamepatwa na majanga mbalimbali wawapo kazini.” Alisema.

Naye Mwalimu Mkuu Msaidizi Shule ya Sekondari Wenda iliyoko Mbalizi,  Mbeya, Neema Ngailo amesema WCF imesimama kwa niaba ya wafanyakazi na waajiri linapotokea suala la mfanyakazi kupatwa na madhila kutokana na kazi.

“Ile namna ya kunifanya nijione kama sijaachwa peke yangu ni jambo la faraja na nitoe wito kwa waajiri ambao bado hawajajisajili au wanalega lega kujiunga na WCF wafanye hima, ni Mfuko unaotoa hakikisho kwa mtumishi pindi anapokumbwa na majanga awapo kazini.” Amesema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, amesema Mfuko umejiandaa kusajili wanachama wengi zaidi kutokana na jitihada za Serikali za kutengeneza ajira kupitia kilimo.

“Tumeungana na Serikali yetu ya awamu ya sita ambayo imekuwa ikipambania sana kutengeneza ajira kwa ajili ya vijana na akina mama kupitia mipango mbalimbali ya kuwaandaa vijana ili kushiriki katika kilimo biashara na pindi watakapoanza shughuli zao na kuajiri, watastahili kuwa wanachama wa WCF.” Amesema.

Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma akitembelea mabanda ya Wanachama wa Mfuko huo

Elimu ya fidia kwa wafanyakazi ikiendelea kutolewa kwenye banda la WCF Viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya.

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Bw. Gerald Mweli (kulia) akifurahia jambo na Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba walipokutana kwenye banda la WCF.

Mkurugenzi Mkuu wa WCF Dkt. John Mduma(wakwanza kushoto), akiwa na Wakuu wenzake wa Taasisi za serikali kwenye kilele chs sherehe za Nanenane jijini Mbeya Agosti 8, 2023.

Maafisa wa WCF wamsikiliza mwananchi aliyetembelea banda la Mfuko huo

Asifa Mfawidhi Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bi. Rose Satta (wapili kulia) na Afisa wa Mfuko huo, Bw. Justin Mwandumbya (kulia) wakitoa elimu kwa mwananchi huyu aliyetembelea banda la Mfuko huo.

Dkt. Mduma akiwa na timu ya WCF.