October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali, wazalishaji saruji waweka mambo sawa

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira,Online

SEKTA ya Ujenzi ni miongoni mwa sekta zinazokua kwa kasi nchini, hii ni kutokana na miradi mbalimbali ya maendeleo inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Uwekezaji, Angellah Kairuki, pamoja na Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa wamefanya kikao cha pamoja na wazalishaji wa saruji nchini kwa lengo la kujadili fursa mbalimbali, changamoto na namna bora ya kukuza sekta ya ujenzi nchini kupitia saruji, kikao kilichofanyika Ofisi za Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), jijini Dar es Salaam.

Katika kikao hicho, mawaziri hao walikutana na kampuni tisa za saruji zikiwemo Dangote Cement.

Camel Cement, Nyati Cement, Mbeya Cement, Kilimanjaro Cement, Maweni Cement, Tanga Cement, Lake Cement, Twiga Cement pamoja na Shirikisho la Wenye Viwanda Nchini (CTI), wakijadili namna bora ya kuendeleza sekta hiyo.

Waziri Bashungwa amewapongeza wazalishaji hao kwa kazi kubwa wanayoifanya na kuwasihi wasipandishe bei ya saruji kiholela hasa kuzingatia kuwa lengo la Serikali ya Awamu ya tano ni kuiona Tanzania inakua nchi ya viwanda.

Wazalishaji hao walizungumzia changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo ikiwemo ubovu wa barabara hasa kipindi cha mvua, unaofanya bei kuwa juu kidogo, upatikanaji wa nishati madhubuti kama gesi, suala la kodi na kuiomba serikali sikivu kushughulikia changamoto hizo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-Uwekezaji, Angellah Kairuki pamoja na Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa wakifuatilia masuala mbalimbali na wazalishaji wa saruji walipokutana kwa lengo la kujadili fursa, changamoto na namna bora ya kukuza sekta ya ujenzi nchini kupitia saruji. Kikao hicho kilifanyika Ofisi za Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Na mpiga picha wetu

Naye, Waziri Kairuki amesema kuwa wizara yake na Wizara ya Viwanda wanafanya kazi kwa ukaribu na kuwatoa hofu wazalishaji hao wa saruji kuwa Serikali ipo pamoja nao na inashughulikia changamoto zao na kuwahakikishia wizara yake yenye dhamana ya uwekezaji itahakikisha inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji hao.

Naye Waziri wa Viwanda na Biashara, Bashungwa aliwahakikishia wazalishaji hao kuwa serikali ina angalia namna bora ya kuhakikisha gesi inapatikana kwa urahisi hasa kwa viwanda vilivyopo Ukanda wa Pwani pia amewahakikishia kuwa changamoto nyingine ndogo ndogo atazishughulikia ndani ya wiki moja ijayo.