May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali kutathmini utayari kukabiliana na maafa

Na Mwandishi Wetu

SERIKALI itaendelea kufanya tathmini ya hiari dhidi ya utayari wake katika kukabiliana na majanga hasa milipuko ya magonjwa na kwamba tathmini zitasaidia katika kukabiliana na milipuko hiyo na kuboresha maeneo mbalimbali yanayolinda afya za watu hapa nchini.  

Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi wakati wa Kikao Kazi cha Makatibu Wakuu Kupitia na Kujadili Rasimu ya Taarifa ya Tathmini ya Hali ya Utekelezaji wa Afya kwa Wote na Utayari wa Kukabiliana na Dharura kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano  wa  Ofisi ya TAKWIMU Jijini Dodoma tarehe 08 Novemba, 2023.

Dkt. Yonazi ameeleza kuwa, upo umuhimu wa kufanya tafiti na tathmini hizo kwa kuzingatia uwepo wa milipuko ya magonjwa mbalimbali kwa ajili ya kuboresha maeneo mbalimbali yanayolinda afya za watu wetu.

“Leo tumekutana na Makatibu Wakuu na wataalam wetu kuangalia namna ambavyo tathmin iliyofanyika katika maeneo mbalimbali ikiwemo upande wa sheria, mifumo na kuona utayari wetu katika maeneo yote muhimu ikiwemo afya, maji, miundombinu, ili kuhakikisha afya ya mtanzania inalindwa, kwa kuwa jambo hili ni la Kitaifa na tunajilinganisha na mataifa mengine ilikuwa muhimu kufanya tathmini hiyo ili kuona matunda ya matokeo katika kuboresha afua za afya,” ameeleza Dkt. Yonazi 

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. John Jingu amesema kuwa Wizara ya Afya imeendelea kujipanga katika kuhakikisha inakabiliana na magonjwa ya milipuko endapo ikitokea.

“Wizara ya Afya itaendelea kuhakikisha huduma za afya zinapatikana sehemu zote nchini, tunaendelea kuhakikisha kunakuwa na vitendea kazi na watenda kazi kwa kuendelea kuajiri watumishi wa kada ya afya na kuwa na utayari na weledi wa kutosha katika kukabili majanga endapo yatatokea,” amesema Dkt. Jingu

Ameongeza kuwa Wizira itaendelea kuajiri watendaji na kuwajengea uwezo kupitia mafunzo mbalimnbali ili kuwa na mbinu za kutosha katika kutoa huduma kwa jamii na kuhakikisha afya za watu wetu zinalindwa.

“Wizara imekuja na mpango wa kuwa na community Health works katika kila kijiji, mtaa hadi mijini ambao watakuwa wanajitolea, sisi tutawawezesha mafunzo na ujuzi katika kuchukua hatua za awali inapotekea suala la maafa.” Amesisitiza.