May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali kusajili vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi 150

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma

SERIKALI imesema itaendelea kuongeza fursa za mafunzo ya amali (elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi) katika vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi.

Hayo yamesema jijini hapa leo,Mei 7,2024 Bungeni na Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Prof.Adolf Mkenda wakati akisoma Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ya mwaka 2024/25.

Ambapo amesema katika kufikia azma hiyo, Serikali itasajili vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi 150 ambapo vyuo vya elimu ya ufundi ni 100 na vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi ni 50, hivyo kuwa na jumla ya vyuo 504 vya elimu ya ufundi na vyuo 885 vya mafunzo ya ufundi stadi.

“Usajili wa taasisi hizo utawezesha kuongeza fursa na kutoa mafunzo kwa kuzingatia viwango na ubora,”amesema.

Aidha amesema serikali itadahili wanafunzi 263,718 wa elimu ya ufundi na mafunzo na ufundi stadi ambapo wanafunzi wa vyuo vya elimu ya ufundi ni 190,518 na wanafunzi wa vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi ni 73,200 sawa na ongezeko la asilimia 23 ikilinganishwa na udahili wa mwaka 2023/24.

Pia itatoa mikopo kwa wanafunzi wa stashahada takribani 10,000 katika fani za kipumbele na zenye uhaba wa wataalam nchini ikiwamo fani sayansi na ufundi na
itadahili wanafunzi 2,089 katika Chuo cha Ualimu wa Mafunzo ya Ufundi Stadi Morogoro – MVTTC ili kuongeza idadi ya walimu wanaofundisha vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi na vyuo vya ualimu wa mafunzo ya ufundi.