May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali kuongeza bajeti ya kilimo nchini

Na: Mwandishi wetu, TimesMajira Online, DAR ES SALAAM.

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Mweli, amesema kuwa Serikali itaendelea kujikita zaidi katika kuongeza bajeti ya kilimo, pamoja na kutatua changamoto za masoko, kuhamasisha matumizi ya taknolojia, pamoja na kuwapatia mitaji vijana, ili kuhakikisha nchi inakuwa na uzalishaji mkubwa wa chakula.

Mweli, ameyasema hayo alipokuwa akizungumza kwenye Mdahalo ulioandaliwa na Taasisi ya Habari Media Brain (MB), Taasisi za Fedha, pamoja na Wahariri wa vyombo vya Habari,  wenye lengo la kujadili fursa na changamoto zitokanazo na mkutano wa AGRF, uliofanyika leo Agosti 30, 2023 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam.

Amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya kilimo imeamua kufanya mageuzi makubwa katika Sekta ya kilimo hapa nchini na kuwa biashara, ili kumsaidia mkulima kuweza kuwa huru katika biashara zake na kujikwamua kiuchumi.

Pia Serikali imewataka wakulima kuweka akiba ya mazao ya chakula kwaajili ya kukidhi familia zao na kuuza ili kujipatia kipato, kutokana na Serikali kufungua uwanja mpana kwa wakulima kufanya kilimo biashara, kwa kuuza mazoa yao nje ya nchi

“Tumefanya kilimo kuwa biashara Kwa kufungua mipaka ili Kila mfanyabiashara awe huru kuuza mazoa yake, lakini kabla hujauza, hakikisha umeweka chakula cha kutosha kwaajili ya kumudu familia “amesema Mweli

Akizungumzia mpango wa ‘Jenga kesho iliyobora’ (BBT) amesema uwepo wa mpango huo, ni kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana, ambapo serikali imeanza kutumia vijana na wanawake kwenye mpango huo.

Amesema katika mpango wa BBT vijana na wanawake wanapatiwa ardhi kwaajili ya kulima mbegu na kuwatafutia masoko.

“Tumefanya tathimini ya kutosha ili kupunguza changamoto ya ajira na vijana, na wengi kutojihusisha na kilimo ndipo tulipojua changamoto na serikali kuanza kulifanyia kazi , ndipo ilipokuja swala la BBT kilimo “amesema Mweli

Ameongeza kuwa changamoto walizokuwa nazo vijana ndio imekua fursa kwenye mpango wa BBT-KILIMO kwa kutoa mitaji kwa vijana, masoko na kuboresha Teknolojia .

Aidha, ameongeza kuwa wakulima wadogo ndio kichocheo cha uweop wa chakula cha kutosha nchini.

Amesema katika mpango wa BBT haujaacha wakulima wadogo ambao tayari walishaingia kwenye kilimo, na kwamba wanaendelea kuwajengea uwezo, na kuboresha miundombinu ili kuweza kulima kitaalam na kibiashara.

Akizungumzia fusa zinazopatikana kutokana na mkutano wa AGRF kwa wakulima wadogo, amesema mkutano huo utakutanisha wadau mbalimbali wa kilimo kutoka mataifa ya Afrika, kwa lengo la mulika mifumo ya upatikanaji wa chakula Barani humo, ambapo wadau wa Sekta ya kilimo wapatao 500 kutoka Tanzania watashiriki.

“Utayari wa nchi kulisha Dunia unachochewa zàidi na wakulima wadogo ambao Serikali inaendelea kuwaboreshea miundombinu ikiwemo kuendelea kuwajengea mabwawa makubwa ya maji Kwa ajili ya kufanya kilimo Cha umwagiliaji na kutoa mbolea za ruzuku Kwa Kila zao” amesema.

Kwa upande wao wadau wa Fedha wakiwemo Benki ya CRDB, NMB, NBC na EQUITY, wamesema kuwa wataendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita, kwa kuinua Sekta ya kilimo, na kuboresha mazingira ya wakulima chini, na kwamba jitihada hizo zimeleta matokeo chanya kwa wakulima na sekta nzima kwa ujumla.

Mkutano Mkubwa wa Mifumo ya chakula Afrika (AGRF) unatarajiwa kufanyika September 5 mpaka 8 mwaka huu, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, huku washiriki zaidi ya 4000 kutoka nje, na washiriki wa ndani zaid ya 500 wanatarajia kushiriki kwenye mkutano huo, utakaotoa fursa nyingi Kwa wadau wa kilimo, pamoja na wafanyabiashara wakubwa na wadogo nchini.