October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Sera ya Elimu toleo la 2023 yakamilika

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema tayari
wamekamilisha Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 na kazi hiyo ilikuwa shirikishi.

Mkenda ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam wakati alipokuwa akizindua Chombo kinachosimamia Elimu ya Dini ya Kiislamu (TISTA) kitakachotoa muongozo wa kufundisha kwa shule za sekondari.

Amesema kazi iliyokuwepo ilikuwa ya kutengeneza sera kupitia sera ya elimu ya mafunzo ya mwaka 2014 lakini baada ya kuipitia imepitishwa na serikali kama sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023 .

Profesa Mkenda amesema sera hiyo iliafikiwa na serikali kupitia Baraza la Mawaziri baada ya Mawaziri wote kumshauri Rais akaikubali.

“Suala la sera ni jambo moja na mitaala lipo tofauti hivyo tulifanya na suala la mitaala ambalo lilikuwa ni shirikishi bahati nzuri sera imepita na mitaala ni kazi ya kiufundi kwa kawaida hata huko nyuma mitaala huwa haiendi kwenye Mabaraza ya Mawaziri inafanywa kiufundi na kupitishwa na kwenda kutumika kwenye shule,”amesema.

Ameongeza kuwa mwaka huu wamefanya shirikishi zaidi kwa sababu mitaala hiyo ilikuwa inahakisi mfumo mpya wa elimu ambao ni tofauti kwa namna kubwa.

“Shule ya msingi sasa ni miaka sita lakini ni lazima mtoto kukaa shuleni kwa miaka 10 ni suala la kisera huwezi kuandaa mtaala ambao hauangalii sera,”amesema.

Pia amesema katika mitaala hiyo kuna masuala ya dini ambayo yana imani zake endapo kutakuwa na mambo hayapo vizuri busara ni kurudi na kusikiliza.

“Mitaala ya dini ni ya kipekee haifanani na somo la kemia dini inavuta hisia na ikitokea tafsiri ambayo sio sahihi tunaweza kuwa na hisia kali dhidi yake tuliliona hilo wakati wa kuandaa mitaala,”amesema Mkenda.

Kwa upande wake Mufti Mkuu wa Baraza la Waislamu Tanzania, Shekhe Abubakar Bin zuber ameishukuru serikali kwa maamuzi sahihi na kuomba kufanyiwa kazi mapendekezo waliyoyatoa ikiwemo kugharamia TISTA.